



Mtandao wa simu za mkononi, Tigo, umezindua huduma mpya ya kuunganisha intaneti katika simu za wateja ijulikanayo kama 'Tigo Jamaa', itakayomuwezesha mteja kutumia huduma hiyo kwa gharama nafuu.
Meneja wa Huduma za Tigo Intaneti, Titus Kafume, alisema wametayarisha timu ya tigo jamaa itakayotembelea maeneo mbalimbali ya nchi, kusaidia wateja kuunganisha simu zao na intaneti kwa haraka na urahisi.
"Tunataka kuongeza uwezo wa wateja wetu katika matumizi ya intaneti kwa kuwasaidia kuwaunganisha kwa urahisi na kwa haraka, hivyo tunawakaribisha wateja kwa wingi," alisema.
Alisema wahudumu hao watakuwa katika baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Mwanza, Arusha, Kilimanjaro na Tanga kuanzia leo.