


.jpg)
Spika wa Bunge, Anne Makinda amesema Tanzania inajivunia uhusiano mzuri kati yake na Japan.
Hayo aliyasema wakati akizungumza katika majumuisho ya ziara yake nchini humo mwishoni mwa wiki iliyopita.
Makinda alisema kuwa, Bunge la Tanzania linaishukuru Japan na Bunge lake kwa kumwalika na ujumbe wa wabunge wake kwenda kujifunza maswala mbalimbali ya kibunge ikiwa ni pamoja na kukuza demokrasia ya kibunge baina ya nchi hizo.
Alisema pamoja na Japan kupitia katika hali ngumu ya kulipuliwa kwa miji yake miwili ya Hiroshima na Nagasaki wakati wa vita kuu ya pili ya dunia, matetemeko ya mara kwa mara na mafuriko ya Tsunami uchumi wake haujayumba kiasi kwamba wameweza kusimama imara kuijenga nchi hiyo.
Makinda naye alitoa mwaliko kwa Spika wa Bunge hilo, Takahiro Yokomichi kuja kutembelea Tanzania ikiwa ni pamoja na kubadilishana uzoefu na wabunge wengine kutoka Bunge la Tanzania.
Akimshukuru Makinda kwa kukubali mwaliko wake, Spika Yokomichi, alisema Japan iliichagua Tanzania miongoni mwa nchi za Afrika kutembelea Bunge lake kwa kuwa ni nchi yenye demokrasia safi na siasa zake zinaimarika kila kukicha .
Yokomichi alisema huo ni mwanzo wa ushirikiano muhimu baina ya mabunge hayo kufanya kazi kwa ukaribu.
Kwa upande mwingine, aliahidi kuishawishi Japan kuendelea kutenga fungu kubwa zaidi kwa lengo la kusaidia sekta mbalimbali za maendeleo Tanzania.