Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula
Mapendekezo ya rufaa za malalamiko ya rafu zilizochezwa katika chaguzi mbalimbali za ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hatima yake itajulikana baada ya kufikishwa katika Kamati Kuu (CC) mpya ya chama hicho.
Baada ya Philip Mangula kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, aliahidi kughuhulikia rufaa hizo ndani ya miezi sita.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema malalamiko pamoja na rufaa zote ambazo Mangula alikuwa akizishughulikia zimekamilika.
Hata hivyo, alisema mapendekezo yake yanasubiriwa kuwasilishwa katika CC ambayo ndiyo itakayotoa mwongozo wa nini kifanyike.
“Kama mnavyojua, katika muundo wetu wa Kanuni ni kwamba Makamu Mwenyekiti anakuwa ni Mwenyekiti wa Kamati ndogo ya Maadili, sasa baada ya kuundwa kwa Kamati Kuu, kila kitu kitakuwa ni sahihi kwa ajili ya kushughulikiwa,” alisema Nape.
Kuhusu kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec), Nape alisema kikubwa ambacho kimekuwa ni gumzo ni suala zima la tatizo la ajira nchini. Alisema katika ajenda zao ambazo walikuwa wakizungumza tangu juzi katika semina, suala la ajira lilichukua sehemu kubwa zaidi.