

.jpg)
Mapigano makali yamezuka kati ya waumini wa dini za Kikristo na Kiislamu katika Kijiji cha Buseresere, Wilaya ya Chato, mkoani Geita, na kusababisha Mchungaji wa Kanisa la Pentecoste Assemblies of God Tanzania (Pagat) , Mathayo Kachila, kuuawa, watu wengine sita kujeruhiwa kwa mapanga na mali zenye thamani ya mamilioni ya shilingi kuharibiwa.
Miongoni mwa waliojeruhiwa, ni pamoja na Msaidizi wa Mchungaji huyo, aliyefahamika kwa jina moja la David, naye amejeruhiwa kwa mapanga.
Mchungaji Kachila alifariki dunia muda mfupi baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Wilaya ya Geita, kutokana na kupata majeraha makubwa kichwani, usoni na shingoni na kupoteza damu nyingi. Pia mali zilizoharibiwa katika vurugu hizo, zimetajwa kuwa ni pikipiki na mabucha ya kuuza nyama.
Mkuu wa Mkoa wa Geita, Said Magalula, na Mkuu wa Wilaya ya Chato, Rodrick Mpongoro, walithibitisha kwa nyakati tofauti kutokea mapigano hayo, kifo na majeruhi.
Kutokana na mapigano hayo, askari polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) walilazimika kutumia mabomu ya machozi kudhibiti vurugu hizo.
Waumini waliohusika na vurugu hizo, wanatoka katika vijiji vya Katoro, Wilaya Geita na Buseresere, Wilaya ya Chato, ambazo zinapakana.
Mapigano hayo yalizuka saa 2 asubuhi baada ya waumini wa Kiislamu kuvamia bucha la kuuzia nyama lililopo katika kijiji cha Buseresere wakimtuhumu mmiliki wake kuuza nyama iliyochinjwa na Wakristo.
Waumini hao, ambao wengi ni vijana, walienda kwenye bucha hilo, huku baadhi yao wakiwa wameficha nyuso zao kwa vitambaa vyeupe, na kuanza kulishambulia kabla ya kuvunja mlango na kuanza kumshambulia mmiliki wake.
Hata hivyo, mmiliki huyo alifanikiwa kuwatoroka, huku akiwa amejeruhiwa na kwamba, waumini hao wanadaiwa pia kuikojolea nyama hiyo na kuinyunyizia vitu, ambavyo havijafahamika.
Askari wa FFU waliongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Chato, Rodrick Mpongoro, na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Geita na Afisa Mwandamzi wa Polisi, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Paulo Kasabago. Akizungumza na NIPASHE jana kwa njia ya simu, Magalula alisema mapigano hayo yalizuka kutokana na mvutano uliopo muda mrefu baina ya waumini wa dini hizo kuhusu haki ya kuchinja.
Hata hivyo, alisema kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira, walifanikiwa kulidhibiti tatizo hilo, hali ikawa tulivu na watu wakaendelea kuishi kwa amani. Alisema mapigano ya jana yalizuka baada ya muumini wa dini ya Kikristo kuchinja na kuweka nyama kwenye bucha.
“Waislamu walipofahamu hilo, ndio zikaanza vurugu,” alisema Magalula. Hata hivyo, alisema majeruhi wawili kati ya sita walitibiwa na kuruhusiwa na hivyo, wamebaki wanne.
Naye Mpongoro alisema serikali haiwezi kuvumilia kuona amani inavunjika, hivyo akaahidi hatua kuchukuliwa baada ya kubaini walioanzisha vurugu hizo. Naye Kasabago akizungumza kwa niaba ya ofisi ya kamanda wa polisi kwenye eneo la tukio alisema mikakati kabambe umewekwa ili kuhakikisha hali ya utulivu na amani vinarejeshwa.