



Nasra Mbwela ana kiu kubwa ya elimu na kumsaidia mama yake mzazi afaulu kimaisha baada ya baba yake kufariki. Umaskini wa mama yake na ukame unaochangia kilimo chao kisiwe na tija akaamua kwenda kufanya kazi za ndani ili apate ada na kumsaidia mama yake.
Amepigwa na kunyanyaswa katika ajira hiyo. Sasa ni mwanafunzi wa sekondari ya Zimbwini wilayani Rufiji na anatamani kuendelea hadi Chuo Kikuu. Makala haya yaeleza zaidi.
Nasra Mbwela, 14, ni mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Zimbwini, wilayani Rufiji mkoani Pwani. Ana ndoto ya kuwa mhasibu.
Baada ya kufiwa na baba yake mzazi mwaka 2009 amekabiliwa na hali ngumu ya maisha yenye misukosuko mingi iliyomlazimisha kufanya kazi za ndani jijini Dar es Salaam. Amezaliwa wilayani Rufiji mkoani Pwani.
Amehitimu elimu ya msingi mwaka 2011 katika shule ya Nyamakonge, Kibiti, wilayani Rufiji. Ni mtoto wa kwanza kwa familia ya Mzee Mbwela. Kwa upande wa mama yeye ni mtoto wa pili kuzaliwa.Ndugu yake ambaye wamezaliwa na baba tofauti anaishi na baba yake.
Baada ya baba yake kufariki mwaka 2009, akabaki akilelewa na mama ambaye ni mkulima wa mazao ya mihogo, mahindi na mengineyo.
Licha ya juhudi za mama yake katika kilimo lakini hali ya ukame ilichangia kufanya wapate mavuno , kwa sababu mazao yanakauka. Hali hiyo ikachangia kuwafanya wawe na maisha magumu hata kujikuta wakishinda na kulala na njaa katika familia yao.
“ Wakati mwingine tunakula au hakuna chakula. Niliumia sana kumuona mama anateseseka.
Akanifahamisha kwamba hana fedha za kugharamia elimu yake . Hali hiyo baada ya kutafakari sana nikaamua kwenda kutafuta kazi za ndani wakati nikisubiri matokeo ya darasa la saba. Mama alisema hata kama nikifaulu hajui kama nitaweza kukosomesha.Mazao yanapandwa na kukauka hana tegemeo jingine,” anasema kwa machungu na kukubujikwa machozi.
Alikwenda jijini Dar es salaam kufanya kazi za ndani mwaka 2011 mara baada ya kumaliza elimu ya msingi. Lengo lake ni kutafuta ada ya kugharamia elimu yake na kumsaidia mama yake kimaisha.
Anasema mama yake alikuwa mkulima wa mazao ya mihogo, korosho, na mahindi aliyokuwa akiyategemea kujikimu na maisha. Hata hivyo, mavuno kidogo kutokana na ukame wa mara kwa mara ulisababisha wawe na matatizo makubwa ya kifedha.
Baada ya miezi mitatu tangu ahitimu elimu ya msingi alienda Dar es Salaam kufanya kazi kwa mama mmoja mfanyabiashara mkazi wa maeneo ya Kigogo. Aliahidiwa mshahara wa sh.40,000 kwa mwezi aliotarajia kuutumia kulipia ada ya shule na kumsaidia mama yake kujikimu kimaisha.
“Nilipofika mwanzoni mama huyo alinipokea vizuri. Lakini kadri muda ulivyozidi kupita ndivyo kazi yangu niliiona kuwa ngumu sana. Nilikuwa siruhusiwi kulala mapema na sipati muda wa kupumzika. Pia ukikosea kidogo tu, mama huyu alikuwa ananifokea sana na kunipiga, glasi ikivunjika kwa bahati mbaya unatakiwa kulipa. Mama huyo pia anadharau sana wafanyakazi wa ndani,” anasema.
Kama hiyo haitoshi, mama huyo akirudi nyumbani mathalani muda wa saa mbili usiku, hutakiwa kumsubiri ale chakula kwa muda anaoutaka hata kama ni saa mbili baadaye ili akimaliza atoe vyombo vya chakula na kwenda kuviosha kisha ndipo aruhusiwe kwenda kulala.
“Wakati nafanya kazi kwa mama huyu mfanyabiashara niliteseka sana. Nilikuwa napigwa vibaya sana.Hakuwa anafundisha au kuelekeza yeye ni kusema kwa ukali na kukutesa hata kuyafanya maisha kuwa magumu.” Anasema kwa masikitiko.
Msichana huyo, aliendelea kufanya kazi hapo hadi Mwalimu Mkuu wa shule ya Nyamakonge alipompigia simu mama yake na kumtaarifu kuwa amechaguliwa kuendelea na masomo ya kidato cha kwanza katika shule ya sekondari Zimbwini,Rufiji.
Mama yake, baada ya kupata taarifa hiyo alifurahi sana licha ya kuwa aliwaza namna ya kupata fedha za kumgharamia kijana wake. Baada ya hapo, alimpigia simu mwajiri wake na kumfahamisha kuwa amefaulu.
Taarifa hizo zilimfikia Nasra wakati anapiga deki na kufanya usafi ndani. Ilikuwa Machi 2012.
“ Baada ya kupata taarifa hizo nilifurahi sana kwa sababu niliona nimejitoa katika mateso niliyokuwa nayapata wakati nafanya kazi za ndani kwa mama huyo,” anasema.
Aliamua kuacha kazi na kurudi nyumbani Kibiti. Huko mama alimfahamisha kuwa hana uwezo wa kumudu gharama zake za elimu.
Hata hivyo, akapata habari njema kutoka kwa mwalimu wake mkuu kwamba kwa sababu darasani alikuwa anajimudu vyema aliombewa msaada katika shirika la Camfed Tanzania linalojishughulisha na kuhudumia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, yatima na wanaotoka katika familia maskini kuanzia elimu ya msingi hadi chuo kikuu.
Mwezi April mwaka 2012 akajiunga na shule ya sekondari ya Zimbwini. Alifurahi sana kuona sasa ndoto zake za elimu zinaanza kutimia. Na ameapa kwamba ana malengo ya kufanya vizuri shuleni hadi afikie ngazi ya chuo kikuu.
Camfed Tanzania walimfadhili mahitaji yote ya msingi ya shule yakiwemo sare za shule , madaftari, ada, viatu, na fedha za matumizi ikiwemo kuwekewa Bima ya Afya kwa ajili ya matibabu na sehemu ya kulala ili aweze kusoma vizuri pamoja na watoto wengine yatima kutoka vijiji mbalimbali wilayani Rufiji.
“Kwa kweli naishukuru sana Camfed Tanzania kunifadhili elimu yangu na naahidi nitaitumia fursa hiyo hadi nimalize vizuri elimu ya sekondari. Pia wameniahidi kunigharamia hadi ngazi ya chuo kikuu kama nitafaulu vizuri katika masomo yangu,”anasema Nasra huku akilia na kufuta machozi.
Masomo anayopenda kusoma ni kemia, hisabati,kiingereza na biolojia.Lengo lake maishani anatamani siku moja afanye kazi ya uhasibu ili aisaidie jamii na hasa mama yake mzazi amwinue kiuchumi.
Mwanafunzi huyo anawashauri wasichana wenzake wanaofanya kazi za ndani, wafanye kazi kwa malengo, wawe wavumilivu na wakiweza kujiendeleza kielimu wafanya hivyo kwa sababu dunia inabadilika , yawezekana wazazi wakafa na kuwaacha wakiteseka hasa kama familia hiyo haina mtu mwenye uwezo au ambaye anajua thamani ya elimu na kuwafanye wabaki wakihangaika .
Kuhusu waajiri wanaopata huduma ya wasaidizi wa ndani, Nasra anawashauri waishi nao vizuri kama watoto wao, wapatiwe mahitaji kama ndugu zao na pia wawe wanawasaidia kufanya kazi inapobidi hiyo itawafanya wahisi kuthaminiwa na kuwa moyo wa kufanya kazi za ndani wakiwa na amani na utulivu.
Akikumbukia mazingira aliyokuwa akifanyia kazi, anasema kwamba alikuwa hapendi kabisa kupigwa. Kero hiyo ilimfanya achukie na kujuta kufanya kazi za ndani licha ya kwamba alikuwa na shida ya kupata ada ya shule.
Shirika la Camfed linafanya kazi katika wilaya kumi za Kibaha, Bagamoyo na Rufiji (Pwani) , Kilolo, Iringa vijijini (Iringa) , Morogoro vijijini, Kilombero,(Morogoro) Pangani na Handeni (Tanga) kuwawezesha kielimu watoto wa kike wanaotoka katika mazingira hatarishi na yatima waliopo shuleni na kuwawezesha kiuchumi wasichana wa vijijini kwa kuwapa mafunzo ya biashara na mitaji .
Mkurugenzi wa bodi ya Camfed Tanzania, Dk. Stella Bendera anasema tangu shirika hilo lianzishwe mwaka 2006 wasichana 3326 wamelipiwa gharama zote za masomo kuanzia elimu ya msingi hadi chuo kikuu katika wilaya hizo.
Pia wanafunzi 10,469 wamenufaika na mfuko wa dharura na tayari wajumbe 177 kati 189 wa Camfed wamepata mafunzo ya uhamasishaji jamii na msaada wa kisaikolojia kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Wajumbe hao ni kutoka wilaya za Handeni, Pangani, Rufiji, Bagamoyo,Kilosa, Kilombero, Morogoro vijijini, Iringa na Kilolo.
Shule 193 zimepata msaada wa vitabu na walimu walezi 157 wamepata mafunzo ya msaada wa kisaikolojia kwa wanafunzi.
Akizungumzia changamoto zinazowakabili katika shirika lake, anasema kuwa baadhi ya wanafunzi wanaofadhiliwa wanaacha shule baada ya kupachikwa ujauzito, ufaulu mdogo, utoro na walimu walezi waliopewa mafunzo kuhamishwa shule.
Changamoto nyingine ni baadhi ya walimu wakuu na walimu walezi kutumia vibaya fedha za walengwa kwa wakuu wa shule.
Mlezi wa wanafunzi katika shule ya sekondari Zimbwini , Latifa Sabuni anasema kwa sababu ya watoto wengi kuishi vijijini katika maisha magumu na kulazimika kutembea umbali mrefu sasa wana mpango wa kupanga nyumba watakayoishi watoto wote wanaofadhiliwa na Camfed Tanzania katika shule yao.
Wanachosubiri sasa ni jengo hilo kuwekewa umeme ili wanafunzi waanze kuishi na kusomea katika mazingira mazuri
Pia anawaomba Camfed Tanzania waongeze kutoa kiwango kikubwa zaidi cha fedha kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi kwa sababu fedha zinazotolewa hivi sasa hazitoshelezi.
“Hebu angalia kila mwanafunzi analipiwa kodi ya nyumba sh 75,000 kwa mwezi. Kwa upande wa vitu vya darasani mathalani madaftari, peni, mkebe wa vifaa vya kupimia wanatoa sh 15,000.Ni vyema wangeongeza hadi sh. 30,000 kulingana na gharama za sasa,” anasema