Thursday Jun 20, 2013
| Text Size
[-]
[+]
Search IPPmedia

Wabunge bajeti 2012/13 iwakomboe wananchi

12th June 2012
Print
Comments
Maoni ya Katuni

Mkutano wa nane wa Bunge la kumi unaanza mjini Dodoma leo mahususi kwa ajili ya kupitisha bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2012/13. Huu utakuwa ni mkutano mrefu utakaokwenda hadi Agosti mwishoni mwaka huu kupitisha bajeti ya kila wizara.

Mkutano huu unafanyika ili kuwapa wabunge fursa ya kutimiza mojawapo ya majukumu yao ya kikatiba. Ibara ya 63 kifungu midogo cha 3 (a), (b) na (c) vinafafanua wajibu wa wabunge wa kuuliza mawaziri na wizara zao maswali; kujadili utekelezaji wa bajeti ya kila wizara; kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu na mfupi unaotaka kutekelezwa ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutunga sheria ya usimamizi wake.

Ni hakika huu ni mkutano muhimu kwa sababu ndiyo utakaoamua mipango ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2012/13, ni katika mkutano huu mawaziri watawajibika kutoa maelezo ya mwelekeo wa kiuchumi wa taifa hili, sababu za kuyumba kwa uchumi, kudorora kwa sarafu ya taifa hili na kwa ujumla kueleza wananchi kupitia wabunge kwa nini hali ya maisha inazidi kuwa ngumu kila uchao na ni nini kinafanyika kubadili mwelekeo huo.

Sisi tunaamini kama ambavyo miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia kwamba wabunge watakuwa makini kuhoji serikali, watadadisi na kuchambua kila mpango wa wizara utakaowasilishwa mbele yao; kwa hakika wabunge hawa watafanya hivyo siyo kwa ushabiki, kuonea mtu au kukomoana au kulindana, ila ni kuhakikisha maslahi ya wananchi yanalindwa vilivyo.

Serikali imekekwisha kusema kwamba kwa mwaka huu wa fedha inatarajia kutumia kiasi cha Sh. trilioni 15, zikiwa ni nyongeza kubwa kutoka bajeti ya Sh. trilioni 13.5 iliyokusudiwa kutumika kwa mwaka wa fedha unamalizaka  mwishoni mwa mwezi huu.

Tunajua pia kuwa serikali inataka kujihakikishia kuwa na akiba ya fedha ya kigeni ya kuweza kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi cha miezi minne na nusu, lakini pia kuhakikisha uchumi unakuwa kwa walau asilimia 6.8 badala ya asilimia 6.4 ya sasa; kuongeza makusanyo ya mapato ya ndani kutoka asilimia 16.9 ya pato la ndani la taifa (GDP) kwa mwaka huu unaomalizika hadi asilimia 17.9 kwa mwaka unaokuja.

Mikakati ni mingi, ila sisi tunataja hiyo hapo juu kwa uchache tu kuonyesha kuwa serikali kwa mwaka wa fedha wa 2012/13 imepania kufanya makubwa; hata hivyo mipango hiyo inahitaji macho na uchambuzi wa wabunge katika kipindi hiki cha mkutano wa Bunge unaonza leo mjini Dodoma.

Mkutano huu wa Bunge unapoanza mjini Dodoma unawakumbusha wananchi juu ya mkutano wa bajeti wa mwaka jana ambao hakika mambo mengi makubwa yaliibuliwa na wabunge, kubwa ni mipango dhaifu hasa katika sekta ya nishati ambayo iliamsha mjadala mkali hadi ikamfanya Waziri Mkuu kuamua kuahirisha mjadala wa makadirio ya matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini ili kwenda kujipanga upya.

Kadhalika itakumbukwa kwamba aliyekuwa waziri wa fedha wakati huo naye alikuwa ametibua umma kwa kutangaza hatua za serikali za kufuta misamaha ya kodi kwa miradi ya taasisi za dini, ambazo kwa hakika zimekuwa mdau mkubwa sana kwa serikali hasa katika kuendesha sekta ya afya na elimu.

Kazi za tasisi hizi hazina ubishi kwamba ni juhudi kubwa ya kuunga mkono mipango ya serikali hasa katika maeneo ambayo hospitali za umma hazipo.

Lakini la muhimu zaidi katika mkutano huu ni serikali kukumbuka kwamba hii ni bajeti yake ya pili baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambao Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoshinda uchaguzi kilikuwa kimemwaga ahadi lukuki katika maeneo mbalimbali nchini, zikijikita katika sekta ya miundombinu kama barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege; sekta ya afya na elimu kutaja hii kwa uchache tu; ni matarajio ya wananchi kuwa ahadi hizi zitaonekana zikifanyiwa kazi kwa kutengwa fedha kwa kazi hizo.

Tunajua vilivyo, wabunge wengi wanajua wajibu wao, wanatambua kuwa wao ni wawakilishi wa wananchi na kwa maana hiyo mkutano huu unaonza leo mjini Dodoma wataonyesha kwa kauli dhabiti na vitendo halisi kwamba wametumwa kuwakilisha wapiga kura wao, cha msingi waanze kuona dalili za maisha bora kwa kila Mtanzania. Kila la heri wabunge.

 

SOURCE: NIPASHE
0 Comments | Be the first to comment