



Serikali imesaini mkataba na serikali ya Canada wa ujenzi wa chuo maalum cha ulinzi wa amani kinachotarajiwa kujengwa nchini mwishoni mwa mwaka huu.
Akizungumza wakati akisaini mkataba huo wa Dola za Canada 650,000 (Sh. 1,005,304,625), Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Shamsi Vuai Nahodha, alisema watazitumia fedha hizo vizuri na wataharakisha ujenzi huo ili kufikia mwakani wanafunzi wawe wameshaanza mafunzo.
“Ujenzi wa chuo hichi utaanza hivi karibuni na chuo kitajengwa Kunduchi jijini Dar es Salaam na tunatarajia ikifika mwisho wa mwaka kitakuwa kimekamilika,” alisema Nahodha.
Aidha, alisema walengwa wa chuo hicho ni pamoja na wanajeshi, askari polisi na raia kwa ujumla na pia watu wa nchi zingine wanaruhusiwa kujiunga.
Balozi wa Canada nchini, Robert Orr, alisema alisema mkataba huo ni moja ya njia ya kuimarisha uhusiano mzuri kati ya nchi yake na Tanzania.