Ebo! Acheni hizo! Mnapenda mno `kuchonga’! Mnabwabwaja hadi inatukifu! Kasema nani kuwa tatizo la walio wengi hapa nchini ni ugumu wa maisha? Acheni kubahatisha!
Mnatuchanganya na misamiati yenu, kuhusu ni ipi `ishu’. Mara mje na mfumuko wa bei, kesho mnaibua kushuka kwa thamani ya sarafu, leo mabadiliko ya tabia nchi nakadhalika, ili mradi tu hamkosi mkwara.
Si kazi serikali ingejitokeza leo na kutangaza hadharani nia ya kutaka kuweka mpango mkakati wa kuwakwamua kimaisha, mngeshindwa kujieleza kinaga ubaga kuwa `ishu’ kwenu ni ipi.
Acheni danadana, pigeni `tageti’. Kimsimamo, kinachopaswa kutajwa kama tatizo la msingi kwa mamia ya Wa–bongo ni kukosekana kwa uwezo wa kipato. Mpo hapo?
Uwezo huo ndio unaoweza kuamua kuwepo au kutokuwepo kwa fursa za ajira na kiwango cha malipo apewacho mtu kwa kazi aifanyayo au huduma aiuzayo; iwe kwenye sekta ya umma au binafsi.
Mwisho wa siku, hali halisi ya malipo hujidhihirisha kwenye uwezo wa mhusika wa kulipia mahitaji yake ya msingi. Hali hii hubadilikabadilika kutokana na sababu anuai ikiwemo upatikanaji chakula, nishati nakadhalika.
Kama hali ya kipato ni duni ni dhahiri kuwa wengi hawatakopesheka katika taasisi za kifedha, kwa kukosa dhamana itakiwayo. Kwa mantiki hiyo, kwenye nyanja za kujiajiri tayari kunajitokeza kikwazo.
Hapa ndipo serikali kupitia Benki Kuu inakotarajiwa kufanya mapitio kwenye viwango vya riba vinavyotozwa kwa mikopo itolewayo na mabenki au taasisi nyingine za fedha.
Aidha, hapa ndo palipo na mahitaji ya serikali au taasisi husika kutoa ruzuku kwa pembejeo na kufuatilia udhibiti wa bei za vitendea kazi muhimu.
Maafisa ugani mathalan kwenye kilimo, uvuvi, ufugaji na ujasiriamali kwenye viwanda vidogovidogo ndo jukwaa lao hili, ili kulifanya eneo hilo kuwa endelevu na lenye tija.
Ni vigumu kwa watu kuwa na malazi bora iwapo kipato chao ni duni. Uwezo wa kujijengea makazi ya kuishi na familia au wanaowajibika kwao utakuwa wa mashaka.
Pamoja na hayo, mamilioni ya wale ambao huuza huduma au kazi zao, hawataweza kuwa na uhakika wa kulipia makazi ya kuishi wao na familia au wanaowajibika kwao.
Kuna ushahidi na uzoefu kuwa wamiliki wa nyumba za kupangisha hudai kodi za pango kwa mwaka. Aidha, kwenye nchi changa. hakuna mamlaka thabiti za kusimamia haki za wapangaji.
Mahakama zimetumika sana kuwaaibisha wapangaji inapotokea kile wakiitacho ni kushindwa kukidhi masharti ya upangaji. Wengi hujikuta wakiwa wahanga hapa kutolewa nje ya nyumba na makampuni ya ufilisi.
Mara nyingine, kuna fursa za mikopo zitolewazo na taasisi kama Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Taifa wa Pensheni kwa Mahirika ya Umma (PPF), Shirika la Taifa la Nyumba n.k.
Fursa zenyewe ni kuwakopesha wananchi nyumba za biashara na makazi, tena baadhi zikitajwa kuwa za bei nafuu, kumbe ni kiini macho. Hiyo ni “kufikirika” kwa kuzingatia jinsi gharama za ujenzi zilivyo juu hapa nchini.
Tunarudi palepale penye uwezo duni kuwa kigingi. Kiuhakika, ni wachache wanaoweza kuzinunua nyumba hizo, hata kama malengo yake ni kuwafikia wenye vipato vya chini.
Ushauri kwa serikali kuhusu haja ya kupunguza au kuondoa kodi kwenye vifaa vya ujenzi umekuwa ni mchakato wa kudumu.
Wenzetu katika nchi za nje, hujenga appartments ambazo hukopeshwa wale ambao wamefikisha umri wa miaka 18, ambao ni umri wa kujitegemea. Huduma kama hiyo huongeza uwezekano wa amani kuwepo.
Aidha, kwa uduni au kukosekana kwa uhakika wa kipato, wengi hawawezi kumudu hata ununuaji wa mavazi kama mahitaji muhimu kwao na wale wanaowajibika kwao.
Pia, kwenye huduma ya afya ni mgogoro, kwani kwa sababu hiyohiyo, wengi hawawezi kumudu gharama za matibabu kwao wenyewe, familia au wanaowajibika kwao.
Ichukuliwe maanani kuwa gharama za afya hazishikiki achilia mbali jinsi familia za kikwenu zilivyo pana, hususan kwa wanaoonekana kwenye nafasi za madaraka.
Kwa Ulaya na Marekani ni tofauti, kwani kuna mafao yatolewayo kila mwezi kwa wote wale wasio na ajira), ili kuwawezesha kuyamudu maisha ya msingi.
Aidha, kwa wenzetu hawahawa, bima za afya zina mchango muhimu sana katika kuwahudumia watu wao, hivyo kuwajengea uhakika wa maisha. Hili ni eneo la kuigwa!
Kadhalika, kutokana na uduni au kukosekana kwa uhakika wa kipato, wengi hawawezi kumudu gharama za elimu, ambayo ni haki na huduma muhimu kwa kila raia.
Mabenki, mifuko mbalimbali na wakfu huko nje hutoa mchango mkubwa sana katika kusukuma hili gurudumu kwa kutoa mikopo au misaada kwa wale wanaoihitaji elimu ya juu.
Ipo haja ya mikakati mipya kwenye suala la mikopo kwa wanafunzi, ili huduma hii iwafikie wale waliotarajiwa tofauti na ilivyo sasa.