

Mkoa wa Morogoro ni mingoni mwa mikoa inayokabiliwa na tatizo la migogoro ya ardhi ambayo mara kadhaa yamelipuka mapigano kati ya wafugaji na wakulima na kusababisha nyumba kuchomwa,watu kujeruhiwa na baadhi kufa.
Mkoa una mashamba pori 220 ya vigogo ambayo hayaendelezwi huku serikali ikishindwa kuchukua hatua za haraka kulipatia ufumbuzi suala hilo.
Mashamba hayo yamekuwa chanzo cha migogoro na kikwanzo cha utekelezaji wa agizo la rais la kuufanya mkoa huo kuwa ghala la taifa la chakula.
Rais Jakaya Kikwete alipofanya ziara mkoani Mororo alitoa agizo hilo la mkoa huo kuufanya kuwa ghala la chakula akiamini kuwa una ardhi na rutuba ya kutosha kuzalisha chakula cha kukidhi mahitaji ya mkoa na nchi.
Morogoro iliingizwa kwenye kundi la mikoa sita inayozalisha chakula kwa wingi nchini.
Mgawanyo mpya wa mikoa uliofanywa hivi karibuni umechangia ongezeko la mikoa hiyo hadi kufikia mikoa saba.
Mikoa hiyo ni Mbeya, Ruvuma, Rukwa, Njombe, Katavi, Iringa, Kigoma na Morogoro.
Ili kufikia kusudio hilo, Morogoro iliweka mpango maalum ujulikanao kama Fanya Morogoro kuwa Ghala la Taifa la Chakula (Famogata).
Hata hivyo, mpango huo umekuwa ukisuasua kutokana na changamoto nyingi ikiwemo ardhi kubwa kumilikiwa na vigogo wanaoshindwa kuiendeleza.
Kaimu Katibu tawala (Uchumi na fedha) mkoa wa Morogoro, Lamiki Noah, aliwaambia wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi iliyotembelea mkoa huo wa Morogoro kuwa mashamba ya vigogo ambayo pia yanajulikana kuwa ni mashamba pori yaliyoachwa bila kuendelezwa kwa miaka mingi yamekuwa kikwazo cha utekelezaji wa Famogata.
Morogoro ina eneo la kilomita za mraba 73,039. Na eneo la hekta 2,226,396 za ardhi zifaazo kwa kilimo sawa na asilimia 30.43 ya ardhi yote.
Kutokana na hali hiyo, ikiwa ardhi ifaayo kwa kilimo itagawanywa kwa usawa kila mkazi wa Morogoro atapata mgao wa ekari 3.12 za ardhi hiyo.
Kutokana na eneo kubwa la ardhi hiyo kuchukuliwa na wawezekezaji na vigogo serikalini, kupanuka kwa makazi ya watu na ogezeko la kasi la idadi ya mifugo kumesababisha migogoro mingi kutokana na uhaba wa ardhi.
Inakadiriwa kuwa mkoa wa Morogoro una zaidi ya ng’ombe 1,222,373 (Sensa 1988). Wataalam wanasema kuwa ng’ombe mmoja anahitaji ekari moja na robo kwa ajili ya malisho yake kwa mwaka.
Kutokana na mahitaji makubwa ya mahitaji ya ardhi ya malisho ya mifugo, kilimo na makazi kumekuwa kunaibuka migogoro mingi hasa baina ya wakulima na wafugaji kwa upande mmoja na wananchi na wawekezaji kwa upande mwingine.
Migogoro hiyo imeshamiri zaidi katika wilaya za Kilosa, Kilombero, Mvomero, Morogoro na Ulanga. Wakulima na wafugaji hugombea ardhi ndogo iliyopo.
Kuwepo kwa mashamba pori zaidi ya 220 ya vigogo umekuwa ukizua vurugu kwa sababu wananchi wengi hukosa ardhi kwa ajili ya kilimo hulazimika kuyavamia mashamba hayo yaliyodumu kwa muda mrefu bila kuendelezwa ili yatumike kuzalisha chakula kwa ajili ya kukidhi mahitaji yao.
Katika siku za hivi karibuni kaya zaidi ya 50 za wakazi wa kitongoji cha Mateteni kata ya Mbigiri wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro walijikuta wakipata hifadhi kwenye mahema baada ya nyumba zao kuvunjwa kwa tingatinga na watu waliodai kuwa ni madalali wa mahakama waliotumwa na aliyekuwa katibu mkuu kiongozi wa utawala wa awamu ya kwanza, Thimos Apio.
Tukio hilo lilikuja baada ya familia hizo awali kukumbwa na mafuriko na uongozi wa mkoa wa Morogoro kuamua wahamishiwe katika eneo la mwinuko lilipo shamba la ( Apiyo) ili kujistiri kwa muda wakati serikali ikifanya jitihada za kuwatafutia eneo jingine la kudumu.
Uvunjaji huo usiozingatia utu umesababisha familia kuishi kwenye mahema yaliyotolewa na aliye kuwa mkuu wa wilaya hiyo, Halima Dendego, baada ya kupata taarifa za tukio hilo.
Mahema hayo yanayotoa hifadhi dhidi ya mvua na jua, lakini hayana staha kwa sababu baadhi ya familia zinalazimika kuishi katika hema moja pasipo kujali jinsi na mahusiano yao.
Licha ya Apiyo, pia wapo viongozi wengi wanaotajwa kumiliki mashamba makubwa mkoani Morogoro wakiwemo, marais wastaafu , Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa.
Wengine ni mawaziri wakuu Fredrick Sumaye na John Malecela, mawaziri, wabunge na
baadhi ya viongozi wa serikali.
Mashamba yanayomilikiwa na vigogo hao yametajwa kuchangia migogoro ya ardhi isiyoisha katika mkoa wa Morogoro, hasa kwa sababu idadi kuwa ya wananchi hawana maeneo ya kulima hali inayowalazimu kuyavamia mashamba ya vigogo hao hususan yasiyoendelezwa.
Hali katika kijiji cha Kikundi tarafa ya Mkuyuni inatatiza kutokana na kukithiri kwa mgogoro wa muda mrefu wa ardhi kutokana na hatua ya wananchi wa kijiji hicho kupinga kampuni ya Morogoro Agro-Enterprises ya mhadhiri wa Chuo kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Prof. Martin Shem kuwaondoa kwa nguvu kutoka katika shamba la Kidago lenye ukubwa wa hekta 1080 linalodaiwa kuwa analimiliki.|
Shamba hilo limekuwa linalimwa na wananchi hao kwa miaka mingi.
Hali hiyo imesababisha familia zaidi ya 300 zilizokuwa zikilitumia shamba hilo kwa zaidi ya miaka 30 kutaabika kwa kukosa eneo la kulima, huku wakiambulia kupigwa na walinzi wa kampuni hiyo na kufunguliwa kesi za mara kwa mara na mmiliki huyo. Wananchi wamekuwa wakilalamikia sana hatua hiyo.|
Mkoa baada ya kubaini kiini cha migogoro mingi ya ardhi uliamua kubainisha mashamba yote yasiyoendelezwa yaliyobakia kama mashamba pori kwa muda mrefu ili kumwomba rais mwenye dhamana ya ardhi kwa mujibu wa sheria kubadilisha matumizi ya mashamba hayo.
Hata hivyo, Rais Jakaya Kikwete wakati akizungumza na waandishi wa habari Ikulu
jijini Dar es Salaam alisisitiza kuwa hatakuwa tayari kubadilisha matumizi ya ardhi yoyote iliyomilikiwa kihalali hadi atakapopewa sababu za kuridhisha za kubadilisha matumizi hayo.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Morogoro Said Amanzi akizungumza katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika mwishoni mwa mwaka jana alisema kuwa rais ametaka orodha ya mashamba yaliyodumu muda mrefu bila ya kuyaendeleza na kuyatathimini upya kabla ya kupeleka tenda kwa rais.
Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Joel Bendera, akitoa msimamo wake kuhusu migogoro ya ardhi katika mkoa wake alisema kuwa, anakusudia kuitisha kikao cha wadau wote ili kwa pamoja watafute ufumbuzi wa migogoro hiyo na kwamba hiyo ndiyo njia pekee itakayosaidia kupunguza madhara yatokanayo na migogoro hiyo.
“Sipendi kufanya mambo nusunusu.Nimemaliza tatizo la ujenzi wa vyumba vya madarasa na watoto wote waliofaulu watakwenda shule. Baada ya sasa nguvu nazielekeza kwenye migogoro ya ardhi. Nataka kukutana na wadau ili kutafuta chanzo na suluhisho la migogoro hiyo,” alisema Bendera.