


.jpg)
Mzozo kati ya Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)kuhusu uhamishaji wa nguzo za umeme kupisha ujenzi wa barabara za mabasi yaendayo kasi, unatafutiwa ufumbuzi, baada ya kuanza kwa mazungumzo.
Msemaji wa Wizara ya Ujenzi, Martin Ntemo, alisema Tanroads na Tanesco wanafanya mazungumzo kuangalia utekelezaji wa zoezi hilo na kwamba taasisi hizo zinafanya mazungumzo kabla ya utekelezaji wa zoezi hilo pindi watakavyomaliza na kukubaliana zoezi hilo litaanza mara moja.
Awali, Tanesco ilisema kuwa kazi ya uondoaji wa nguzo hizo linatakiwa kufanywa na Tanroads. Hata hivyo, Tanroads ilipoulizwa, ilisema jukumu hilo ni la Tanesco.
Mtendaji Mkuu wa Tanroads, Patrick Mfugale, alisema wao hawahusiki na suala la uamishaji wa nguzo na kwamba kazi hiyo inatakiwa kufanywa na Tanesco.
Awali, Meneja Mawasiliano wa Tanesco, Badra Masoud, alisema kuwa zoezi la kuhamisha nguzo linatakiwa kufanywa na Tanroads kupitia mkandarasi wake na kumlipa. Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, hivi karibunialitoa siku saba kwa Tanesco kuhamisha nguzo kupisha mradi huo.