


.jpg)
Serikali inatarajia kutoa Shilingi bilioni 8.2 kwa ajili ya ruzuku ya pembejeo ya dawa za kuua wadudu katika zao la pamba nchini.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Profesa Jumanne Maghembe, alisema hayo jijini Dar es Salaam jana wakati akifungua mkutano wa kujadili namna ya kuongeza nguvu katika uzalishaji wa zao la pamba uliowahusisha wadau kutoka mikoa mbalimbali.
Alisema fedha hizo zitaanza kutolewa hivi karibuni na kwamba lengo lake ni kuwawezesha wakulima wa zao hilo kuzalisha zaidi na kuongeza kipato.
Aidha, Profesa Maghembe aliwataka wakulima kujiingiza katika kilimo cha mkataba ili waanze kulima pamba mpya inayojulikana kwa jina la kitaalam Cotton BT kutokana na ubora wake wa kuzalisha.
Mbali na ubora wake, lakini pia alisema uzalishaji wake ni mkubwa kuliko ule wa pamba inayolimwa sasa.
Mkurugenzi Mtendaji Bodi ya Pamba, Marco Mtunga, alisema endapo wakulima wengi watajihusisha na kilimo cha mkataba kitawasaidia kupata zana bora za kilimo na uzalishaji wao utaongezeka zaidi.