


.jpg)
Ofisi ya Askofu wa Kanisa Anglikana Tanzania, Stanley Hotay, juzi ilivamiwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi na kupora fedha taslimu Shilingi milioni nane na vitu vingine ambavyo thamani yake haijajulikana, kisha kufyatua risasi hewani na kutokomea kusikojulikana.
Habari zilizopatika jana jioni na kuthibitishwa na askofu huyo, zimedai kuwa watu hao waliokuwa na bastola, walivamia ofisi hizo za shirika lisilo la kiserikali la HERE’S Life juzi mjini hapa majira ya mchana muda mfupi baada ya kesi ya madai ya kupinga kusimikwa kwa askofu huyo kuahirishwa.
Akizungumza kw anjia ya simu kutoka mjini Dodoma, Askofu Hotay alisema hawezi kuhusisha tukio hilo na kesi ya madai inayomkabili na kuviomba vyombo vya dola kuchukua hatua na kufanya uchunguzi wa kuwabaini wahusika.
Naye mmoja wa mashuhuda ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema kuwa kabla ya kufanyika kwa tukio hilo, mhasibu wa ofisi hiyo, Neema Mbonea akiwa na dereva walitoka benki na waliporudi ofisini, walivamiwa na watu wawili na kuchukua mfuko uliokuwa na fedha hizo kabla ya kumpiga kwa nondo mhasibu huyo katika bega lake la mkono huku mmoja wao akiwa na bastola.
Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Arusha, Lebaratus Sabas, alipoulizwa kuhusu tukio hilo alikana kufahamu tukio hilo na kudai kuwa hakuwa ofisini kwake na yuko katika msafara wa Rais Jakaya Kikwete, aliyekuwa mjini Moshi juzi kenye sherehe za kilele cha siku ya mazingira duniani zilizofanyika kitaifa mkoani Kilimanjaro.