Wednesday Jun 19, 2013
| Text Size
[-]
[+]
Search IPPmedia

Ndiyo jirani wametusaliti, lakini tujifunze

1st June 2012
Print
Comments
Maoni ya Katuni

Wizara ya Maliasili na Utalii juzi ililazimika kutoa tamko la kusahihisha habari za upotoshaji ambazo ziliandikwa na vyombo vya habari vya Kenya na kueleza kuwa Zanzibar kumechafuka na kwa maana hiyo siyo salama kutembelewa na watalii.

Hatua hii ni ya kusafisha hali ya hewa ambayo imechafuliwa na vyombo hivyo kwa nia ya ama kuwatisha watalii waliokuwa wanapanga kutembelea visiwa hivyo, au ambao tayari walikuwa njiani kuelekea Zanzibar.

Habari hizo za kupotosha na kujenga taswira mbaya dhidi ya Zanzibar nia yake siyo kitu kingine ila ni kutaka kuvutia watalii kwenda Kenya na kuikwepa Zanzibar.

Kwa vyovyote itakavyotazamwa, baadhi ya vyombo vya habari vya Kenya katika suala hili vilikuwa na ajenda moja tu, kunufaika na tukio la Jumamosi, Jumapili na Jumatatu lililotokea visiwani Zanzibar ambako vurugu ambazo hata hivyo hazikugusa vivutio vya utalii moja kwa moja wala kuua au kujeruhi mtu, zilitokea.

Wakati vyombo hivyo vikishikilia bango tukio la vurugu za Zanzibar, nchini mwao kulitokea mlipuko mkubwa ambao ulitikisa jiji la Nairobi, lakini halikupewa nafasi kubwa kama ambavyo ilikuwa kwa Zanzibar. Tukio la Nairobi linaelezwa kuwa ni shambulizi la kigaidi. Halikupigiwa debe sana, nia ilikuwa kulinda mambo yao yasiparaganyike.

Tunachukua fursa hii kusema wazi kuwa nia ya vyombo vyote vya habari vya nje vilivyoeneza habari hizi kupitiliza kwa nia ya kuwaogopesha wageni wanaotembelea Zanzibar siyo nzuri kwa Wazanzibari na kwa Watanzania wote kwa ujumla.

Hata hivyo, mwelekeo huu wa kuripoti habari hizo kwa vyombo vya habari vya nchi jirani ambayo tumo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ifungue macho na masikio ya Watanzania kwa ujumla wetu ili kuchukua hadhari juu ya kulinda na kutetea maslahi yetu kama taifa.

Kadhalika, kwa wote ambao wamekosa ufahamu juu ya madhara ya vitendo vya uvunjifu wa amani wakitoa visingizio vya ovyo kabisa kuhusu Muungano, na kujidai kuwa wanatafuta haki, wajue kwa hakika wanachofanya ni mchezo mbaya siyo kwa hao wanaowaandama na kuyujumu ama nyumba zao za ibada au vitegauchumi vyao, ila wanajenga anguko lao wenyewe.

Jana tumemsikia Rais wa Zanzibar akielezea kwa masikitiko makubwa juu ya vurugu hizo na kutoa onyo kwamba uvumilivu wa serikali umefikia ukomo, kwamba sasa atakayeendesha vitendo hivyo atashughulikiwa mara moja; lakini pia amewakumbusha Wazanzibari juu ya umuhimu wa sekta ya utalii kwa ustawi wa uchumi wa Zanzibar.

Sekta hiyo inabeba asilimia kubwa mno ya mapato ya serikali, ni sawa na mshipa mkuu wa fahamu kwa maana ya kuendesha uchumi wa Zanzibar, bila utalii Zanzibar haiwezi kusimama, lakini pia bila utulivu utalii nao hauwezi kuwepo.

Katika muktadha huo, pamoja na kijicho cha jirani zetu na kutuombea mabaya ili wao wanufaike, ni vema wale wote wanaojifanya kuwa ni wakereketwa wa mambo wajifunze kufanya mambo kwa staha, kufuata sheria na kutambua wakati wote kwamba katika dunia ya sasa vurugu ndani ya jamii hazijengi nchi, ni maafa ambayo huleta madhara kwa wote.

Kujenga nchi ni kazi ngumu, zito na inayochukua muda mrefu, lakini kuisambaratisha nchi ni suala la muda mfupi sana.

Vurugu za siku tatu zilizotokea Zanzibar zingetosha kabisa kuizamisha Zanzibar katika tasnia ya utalii kama siyo juhudi za nguvu za dola kupitia Jeshi la Polisi katika kuwadhibiti waliokuwa wanaendesha vurugu kwa kisingizo chochote kile.

Juzi katika safu hii ya tahariri tulisema bila kumung’unya maneno kwamba vurugu hazikubaliki Zanzibar na kwa hakika hazina nafasi katika taifa hili, kama mwenye duku duku lake hawezi kutumia mifumo ya kisheria iliyowekwa kudai, basi ajue kuwa hana hoja na asitumie udhaifu wake kuvuruga nchi.

Ni kweli jirani zetu wamekosa uungwana kwa kupaza sauti kupita kiasi juu ya matatizo yaliyotokea Zanzibar ingawa kwao kulikuwa na jambo baya hata kuliko hili, lakini hawakulipigia sana kelele kwa sababu wanajua madhara yake kwa uchumi wa nchi.

Hata hivyo, ni angalizo zuri tumepewa kama nchi, hasa wale wanaoongoza vikundi mbalimbali katika jamii kutambua wakati wote kuwa hakuna mweye kuionea nchi huruma zaidi ya mwananchi wake, hivyo tuwe na kiasi na hatua tuchukuazo kudai haki hizi.

Mwenye kujisifu kwa sababu ameitumbukiza nchi yake katika maangamizi ni mwehu, juha asiyestahili kuishi, kwa kuwa mwisho wa yote kila haki tunayodai inalenga kuleta maisha bora zaidi kwa mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla wake, vurugu hazituhakikishia neema yoyote, tuachane na ujuha.
 

SOURCE: NIPASHE
0 Comments | Be the first to comment