


.jpg)
Baraza Kuu la Chama cha Wafanyakazi wa Reli (Trawu), limeitaka serikali kuiwajibisha mara moja Menejimenti ya Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara), kwa kushindwa kutekeleza ahadi ya kuwalipa mishahara wafanyakazi wake.
Katibu Mkuu wa chama hicho, Erasto Kihwele, alisema mejimenti hiyo imeshindwa kuheshimu ahadi iliyotoa kwa Waziri wa Uchukuzi, Omary Nundu, alipotembelea ofisi za mamlaka hiyo kutafuta suluhu ya mgomo wa wafanyakazi.
Kihwele alisema katika kikao cha baraza hilo kilichofanyika hivi karibuni mjini Morogoro, pia wajumbe wamesikitishwa na kulaani kitendo cha menejimenti ya Tazara Mkoa wa Mbeya kuwawajibisha viongozi wa Trawu mkoani humo, kwa madai kuwa wamechochea mgomo wa wafanyakazi na kutaka adhabu hiyo ifutwe mara moja.
Aidha, Trawu imeutaka uongozi wa mamlaka hiyo kuachia ofisi zao ili zikaimiwe na watu wengine wenye uwezo na kutoa nafasi ya kufanyika uchunguzi wa haki na limeitaka serikali kulipa mishahara ya wafanyakazi wa Tazara ili kuokoa maisha yao.
Kihwele aliongeza kuwa baraza hilo pia linaiomba serikali itengue Sheria ya Reli namba 4 ya mwaka 2002 iliyounda Kampuni ya Miliki ya Rasilimali za Reli (Rahco) ili kuondoa urasimu uliopo kati ya kampuni hiyo na Shirika la Reli (TRL) hali inayozorotesha utendaji wa kazi.