


.jpg)
Katibu Uenezi wa Chama cha NCCR-Mageuzi Mkoa wa Arusha, James Ndarivoi, amejiuzulu wadhifa huo kwa kupinga vitendo vinavyofanywa na viongozi chama hicho Makao Makuu kwa kumfukuza uanachama Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila.
Mbali na kujiuzuku, akejitoka katika chama hicho na kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa maelezo kuwa ndicho chama pekee chenye nguvu na hoja za ukweli kwa upande wa upinzani.
Ndarivoi alisema kabla ya kuchukua uamuzi huo, aliwasiliana na viongozi wake makao makuu ya chama hicho kutaka kufahamu kikao cha Halmashauri Kuu (NEC) ya NCCR-Mageuzi kiliwakilishwa na wajumbe gani kwa kuwa wao kama Mkoa wa Arusha hawakuitwa katika kikao hicho.
“Sasa kama wanakata simu wanafahamu ni kosa wamefanya huo uamuzi wa kumfukuza huyu Mbunge aliyekuwa analeta chachu katika chama, imefanywa kwa hila na imetushtua na kutusikitisha,” alisema na kuongeza: “Ni maamuzi batili yaliyofanywa na wachache kwa maslahi yao binafsi bila kuwepo kwa wajumbe wa Mikoani kama katiba yao inavyosema.”
Ndarivoi alisema Kafulila alikuwa na haki ya kuhoji kuhusu ruzuku inayoishia makao makuu, ila kwa sababu ya ufisadi wa watu wachache, hawakutaka kuhojiwa hilo na kuamua kumtimua.
Alisema kuwa yeye na jopo la wanacahama kadhaa wa Mkoa wa Arusha wanatarajia kujiunga na Chadema, ili kukipa nguvu zaidi kwa kuwa ndicho chama chenye msimamo na kisichopenda utani.
Aidha, alisema kuwa anasikitishwa sana na vitendo vya vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani nchini, kwani badala ya kujenga demokrasia komavu na upinzani imara, wao wanadidimiza kwa kujipendekeza kwaChama cha Mapinduzi (CCM) au kwa maslahi yao binafsi.
“Kama tutafanya hivi hatutajenga vyama hivi na Chadema kitazidi kupaa juu kwa sababu wananchi wa sasa wanaona matendo ya kila chama jinsi yalivyo na wao wana uwezo wa kuamua, hivyo natoa wito kwa wanachama wenzangu wa Mkoa wa Arusha kuhama chama hiki na tuhamie Chadema ili kujenga upinzani imara,” alisema Ndarivoi.