


.jpg)
Benki ya Dunia imetoa Sh. bilioni 159 kwa Tanzania kwa lengo la kuisaidia kuboresha mazingira ya kujenga uchumi imara na kuboresha ajira kwa wananchi.
Akisaini mkataba huo jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Fedha, Mustapha Mkulo, alisema kati ya sehemu ambazo pesa hizo zitagawanywa ni katika ardhi na miundombinu hususani bandari.
Alisema kupitia fedha hizo, wanatarajia kuboresha upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya kuongeza uwekezaji ambao kwa namna moja utasaidia kuongeza ajira hata kuongeza ukuaji wa uchumi.
Alisema wana uhakika pesa hizo zitasaidia kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa ardhi kwa wawekezaji na kuifanya sekta binafsi kuwa ndio kichocheo kikubwa cha uchumi.
Alisema zitasaidia pia katika kuboresha na kurahisisha upatikanaji wa mizigo katika bandari hapa nchini.
Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia Afrika Mashariki, Philippe Dongie, alisema wameamua kusaidia katika sekta hizo kwa sababu ni mojawapo ya sekta muhimu zinazochangia katika ukuaji wa uchumi.