|
Bibi aliyetelekezwa na wajukuu aomba msaada...hana chakula wala makazi
2005-07-26 15:45:44
Na Martha Colman, Mbezi
Bibi mmoja ambaye ana matatatizo ya miguu, aliyejitambulisha kwa jina la Swaumu Ramadhani , 60, mkazi wa Mbezi Luisi, Jijini, anaishi kwa taabu kubwa kutokana na kutokuwa na nyumba ya kuishi.
Bibi huyo ambaye anatembelea magongo, amesema hali yake inazidi kuwa mbaya siku hadi siku kutokana na kutokuwa na pesa ya chakula wala nguvu za kuhangaika kutafuta riziki kwa kulima vibarua.
Amesema ulemavu huo aliupata baada ya kugongwa na baiskeli.
Mbaya zaidi anasema hivi sasa anaishi na wajukuu zake wawili ambao wazazi wao hawana mbele wala nyuma.
Niliwachukua wakati nikiwa mzima ambapo nilikuwa naweza kulima vibarua...lakini hivi sasa sina jinsi ya kuwahudumia, akasema.
Amesema kuwa anaishi kwa kutegemea misaada ya watu wanaopita na kumwonea huruma kutokana na hali yake.
Wajukuu hao mmoja ana umri wa miaka mitano na mwingine miaka minne.
Amesema kijana aliyemgonga mpaka leo hamfahamu kwa kuwa ilikuwa ni mida ya jioni na baada ya kumgonga hakusimama kumpa msaada wowote ule.
Nilikwenda hospitali ya Serikali Mbezi na kupata matibabu na kuambiwa mguu umevunjika kwa ndani na wakanishauri nikatafute hela ili niende Muhimbili nikafanyiwe operesheni, akasema.
Hata hivyo amesema kutokana na hali yake hakuweza kwenda Muhimbili kuonana na madokta zaidi ya kukaa tu nyumbani na kusubiri kuomba msaada huku na kule bila mafanikio yoyote yale mpaka leo .
Mimi naishi kwenye shamba la mtu tu, nilijengewa nyumba ya nyasi na kijana mmoja anayetambulika kwa jina la Sefu, baada ya kunikuta nahangaika mtaani bila kufahamu pa kwenda baada ya kutoka kijijini kwetu Dodoma, akasema.
Amesema binti yake alimtoroka na kumwachia watoto ambao hajui atawalisha nini.
Baba wa watoto hawa simfahamu na hapa mjini sina ndugu yeyote...naomba msaada ndugu zangu, akaomba.
|