|
Maalim Seif apata ajali
2005-07-26 15:49:36
Na Janneth Kiure, Kibaha
Gari la Katibu Mkuu wa chama cha wananchi CUF, Maalim Seif Sharif Hamad limepata ajali. Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Pwani, Ally Mbilikira, ameliambia gazeti hili mapema leo kuwa ajali hiyo ilitokea jana saa 2:00 asubuhi huko Makole kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo, mkoani Pwani.
Amesema Maalim Seif alikuwa anakwenda Handeni mkoani Tanga akitokea Jijini Dar es Salaam.
Akielezea tukio hilo, Kamanda Mbilikira amesema gari hilo lilimgonga mpanda baiskeli mmoja aitwaye Eliamini Eujeim, 20, mkazi wa eneo hilo la Makole.
Akasema kijana huyo amejeruhiwa vibaya.
Kwa mujibu wa Kamanda Mbilikira, Maalim alikuwa kwenye gari lenye nambari za usajili T 215 AEC aina ya Nissan Patrol lililokuwa likiendeshwa na dereva Ally Said, ambaye ni mkazi wa Pemba.
Hata hivyo amesema Katibu Mkuu huyo wa CUF ambaye ndiye mmiliki wa gari hilo, hakujeruhiwa.
Kufuatia tukio hilo, Kamanda amesema dereva huyo anashikiliwa na polisi wakati upelelezi unaendelea.
Majeruhi huyo amelazwa katika hospitali teule ya Tumbi kwa matibabu.
|