|
Sakata la Uwanja wa Fisi si lelemama, Serikali yakiri
2006-08-28 17:32:03
Na Abdul Mitumba, Kinondoni
Serikali wilayani Kinondoni Jijini Dar es Salaam, imesema inahitaji muda zaidi wa kushughulikia kwa kina zoezi la kuondoa changudoa na makahaba eneo la Uwanja wa Fisi.
Zoezi hilo lililoanza baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bwana Abbas Kandoro kuzuka katika eneo hilo na kutoa amri ya kukomeshwa kwa kila kitu kichafu kama njia pekee ya kumaliza tatizo hilo.
Ili kufikia malengo, baadaye iliundwa kamati ikishirikisha baadhi ya wamiliki wa madanguro hayo na kupewa wiki moja iwe imemaliza tatizo hilo.
Mratibu wa kamati hiyo, Bibi Josephine Matiro amekiri kuwepo kwa ugumu huo, ingawa amesema bado wanaendelea na mapambano.
Bibi Matiro, ambaye pia ni Katibu Tarafa ya Kinondoni, amesema ili kufikia malengo thabiti, kamati yake imelazimika kumjumuisha mkuu mpya wa wilaya ya Kinondoni, Bw. Phabian Massawe katika vita hiyo ngumu.
Kazi ya Uwanja wa Fisi siyo lelemama, kwa wakati huu naomba tuliache kwanza hadi mwishoni mwa mwezi huu bila shaka litakuwa na sura nzuri, amesema.
Kauli hiyo ya Bi. Matiro inafanana na iliyowahi kutolewa na aliyekuwa Kaimu Mwenyekiti wa mtaa wa Muungano unaogusa eneo hilo, Bw. Filberth Masenene ambaye alisema kamati iliyoundwa kushughulikia suala hilo imefeli.
Pamoja na mambo mengine, eneo la Uwanja wa Fisi lililopo katika Manispaa ya Kinondoni liliamriwa kufungwa baada ya kubainika linatumika kwa biashara za ngono kwa vijana wadogo, uuzwaji wa pombe haramu na matumizi ya kupindukia ya dawa za kulevya.
|