|
Binti acharangwa visu kwa wivu
2006-10-19 20:40:49
Na Magreth Simba, Temeke
Msichana Juliana Daniel amelazwa katika Hospitali ya Amana Ilala Jijini Dar baada ya kucharangwa visu kifuani na mabegani na mtu anayetajwa kwa jina moja la Bw. Kessy.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala Bw. Masindoki Masindoki amesema tukio hilo limetokea huko Stakishari Ukonga Jijini.
Amesema Bw. Masindoki kuwa chanzo cha Juliana kuchomwa visu kinasemekana kuwa ni wivu wa kimapenzi baada ya mwanaume huyo kumkuta akiwa amesimama na mwanaume mwingine aliyetajwa kwa jina la Bw. Jacksoni Membi.
Amesema hata Jaksoni pia alijeruhiwa na visu hivyo lakini ametibiwa na kuruhusiwa.
Akasema Bw. Masindoki kuwa mtuhumiwa Kessy anashikiliwa na Polisi na uchunguzi unaendelea.
Katika tukio jingine, nyumba moja inayomilikiwa na Meneja wa kampuni ya Royal Shipping Campany iliyopo Tegeta imeteketea kwa moto na uchunguzi wa chanzo cha ajali hiyo unaendelea.
|