|
Wanaosaka viza za Marekani kwa ujanja ujanja sasa kuula wa chuya
2006-10-21 14:20:27
Na Emmanuel Lengwa, Msasani
Watu wenye tabia ya kufanya udanganyifu ili kujipatia viza za kuingia nchini Marekani sasa walie tu kufutia mwarobaini wao kuchemka.
Mwarobaini huo pia utawanasa wale wenye tabia ya kukimbilia nchi nyingine kuomba visa ya nchi hiyo huku wakiwa wamebadilisha majina, picha na hata pasipoti.
Taarifa iliyotolewa na ubalozi wa nchi hiyo hapa nchini imesema udhibiti huo wa hali ya juu utawezekana kutokana na na Serikali ya nchi hiyo kuanzisha mpango kabambe wa kuwabana wajanja wenye kawaida ya kujipatia viza zao hizo kwa njia ya udanganyifu.
Katibu wa Ubalozi wa Marekani anayeshughulikia masuala ya Uhamiaji Bw. Robert Hannan, amesema balozi zote za Marekani sasa zimeunganishwa na mtandao maalum wa kompyuta kwa lengo la kuhakikisha wajanja hao hawapati upenyo.
Amesema mtandao huo una programu spesho inayotambua picha na alama za vidole za mtu aliyekwisha omba viza kwa mara ya kwanza mahali popote katika balozi za nchi hiyo duniani kote.
Siyo rahisi sura na alama za mtu yuleyule kukubalika kwenye programu hii... hivyo mtu aliyekwishaomba viza mahali popote halafu akakataliwa kwenye balozi zetu, tutamfahamu kwa urahisi, akasema Bw. Hannan.
Kadhalika Bw. Hannan alizungumzia masharti ya kuingia Marekani.
Bw. Hannan ameyataja baadhi ya masharti kwa waombaji kuwa ni pamoja na kutokuwa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi ambao wao, amesisitiza kuwa kamwe hawatapewa viza hizo kwa sababu nchi yao iko makini katika kulinda afya za wananchi wake.
Kila nchi lazima iweke taratibu zake za uhamiaji kwa maslahi ya taifa... na sisi utaratibu wetu ndio huo, hatutatoa viza kwa watu wenye maradhi ya kuambukiza, akasema Bw. Hannan.
|