|
Pindupindu lawabwaga kitandani wakazi 27 Jijini
2006-10-21 14:21:33
Na Humphrey Kadege, Jijini
Jumla ya wagonjwa 27 wa kipindupindu kutoka katika Manispaa za Jiji la Dar es Salaam, wamelazwa katika hospitali mbalimbali za Jijini.
Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Jiji, Dokta Deo Mtasiwa wakati akiongea na Alasiri ofisini kwake.
Dk .Mtasiwa amesema miongoni mwa wagonjwa hao, 14 wanatoka Manispaa ya Ilala, katika maeneo ya Buguruni, Vingunguti , Kitunda na Ukonga.
Kwa upande wa Manispaa ya Kinondoni, wagonjwa hao amesema wanatoka katika maeneo ya Tandale, Manzese, Ubungo, Kigogo, Mabibo, na Makulumla, ambapo katika Manispaa ya Temeke maeneo yenye wagonjwa ni Tandika Keko na Sandali.
Aidha amesema kuwa Manispaa zote tatu zimefanya ukaguzi wa maeneo katika majengo na biashara, kwa kufanya oparesheni ya usafi wa masoko, barabara na mifereji pamoja na kudhibiti madampo yasiyo rasmi.
Pia ametoa wito kwa wananchi kuchemsha maji ya kunywa, kuoshea vyombo na juisi itengenezwe kwa maji safi na salama.
Amepiga marufuku tabia ya baadhi ya watu kutiririsha maji machafu, kuuza vyakula mitaani, pamoja na kutupa taka kwenye mifereji.
Katika kupambana na ugonjwa huo, Halmashauri ya Jiji imetoa dawa katika vituo vyote vinavyohudumia wagonjwa wa kipindupindu, ambavyo ni Buguruni, Tambuka Reli na Mburahati.
|