|
Answar wala Iddi yao
2006-10-23 17:26:13
Na Mwandishi Wetu, Jijini
Kama ilivyokuwa wakati wa kuanza kwa mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, Waislamu wameendelea kusigana tena kuhusu sherehe za siku ya Idd-el-Fitr ambapo leo, mamia miongoni mwao wamejimwaga kwenye maeneo tofauti Jijini Dar na kuswali swala ya Iddi.
Leo pale katika viwanja vya Jangwani, Tandika, Tabata, Kinondoni Biafra na maeneo mengine kadhaa, mamia ya Waislamu wanaofahamika zaidi kama Answar Sunna wameonekana wakiswali sala hiyo inayoashiria kumalizika kwa mfungo wa Ramadhani huku maelfu wengine wakiendelea kusubiri Idd hiyo kesho kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa kabla na chombo chenye mamlaka ya kutangaza sikukuu za Kiislamu nchini, yaani Baraza Kuu la Waislamu Tanzania, BAKWATA.
Pale katika viwanja vya Jangwani, Waislamu walianza kwa kuvuta takbira na nyiradi nyinginezo kadhaa. Kisha muda mfupi kabla ya kufikia muda wa swala amabo ni saa 1:30, kukatokea mvua za rasharasha zilizofanya zoezi hilo lisite kidogo ambapo jenereta iliyokuwa ikisaidia matumizi ya kipaza sauti ikatafutiwa hifadhi, kisha ilipotimu mishale ya saa 1:33, swala hiyo ikaswaliwa.
Wakati huohuo, BAKWATA ilishatangaza kuwa mwaka huu, swala ya Idd kitaifa itaswaliwa kitaifa saa 1:30 katika Msikiti wa Bondeni Jijini Arusha kesho.
Sambamba na swala hiyo, pia Baraza la Idd litafanyika mkoani humo ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bw. Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Taarifa hiyo ilisema kuwa sikukuu ya Idd itakuwa leo ama kesho kufuatana na mwandamo wa mwezi ambapo kwa sababu leo Baraza hilo halikutangaza Idd, maana yake ni kuwa kesho ndo siku yenyewe.
Jijini Dar, Baraza la Idd huenda likafanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja ama kwenye ukumbi wa hoteli ya Starlight.
|