|
Asasi yapigia debe yatima kuhusu elimu
2006-12-27 18:37:17
Na Mary Wejja, Mikocheni
Serikali na Asasi zote zisizo za Kiserikali, zimetakiwa kuwasaidia yatima na watoto waishio katika mazingira magumu kwa nguvu zote ili wapate elimu na hatimaye iweze kuwakomboa kimaisha na pia waweze kutoa mchango wa maendeleo kwa taifa.
Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Asasi Isiyo ya Kiserikali ya inayotoa huduma ya Elimu kwa yatima na kuhudumia wazee la Home and Care for Aged and Orphans (HOCOA), Bw.Emmanuel Malekeno, wakati akizungumza na Alasiri ofisini kwake hivi kribuni.
Serikali na asasi zisizo za kiserikali zianzishe shule maalumu kwa ajili ya yatima na watoto waishio katika mazingiora magumu... hilo ni jambo la msingi zaidi katika kuwafanya waweze kukabiliana na changamoto za maisha hapo baadaye, akasema Bw. Malekano.
Akaongeza kwa kusema kuwa misaada mingi inayotolewa sasa kwa yatima ni ya chakula, malazi na mavazi, ni sehemu ndogo tu ya yale wanayoopaswa kuwa nayo maishani, hivyo ni bora suala la elimu likapewa kipaumbele cha kwanza kwao.
Na kwa kutambua umuhimu wa jambo hilo, Bw. Malekeno amesema asasi yake ya HOCOA imejenga shule maalumu ya sekondari kwa ajili ya yatima na kuiita kwa jina la New Horizon.
Tunaomba wwatu wengine wajitokeze na kutuunga mkono katika ujenzi wa shule hiyo ambayo sasa ina wanafunzi 38 na baadhi wamefanya mtihani wa kidato cha pili mwaka huu... tuna uhaba wa madarasa yatakayotuwezesha kuchukua yatima wengi zaidi na hivyo ni vyema tukaungwa mkono katika nia yetu hii ya kusomesha yatima na watoto waishio katika mazingira magumu, akasema Malekeno ambaye pia amedai kuwa hivi sasa wanasaka msaada wa shilingi milioni 150 ili wakamilishe sekondari ya bweni ya madarasa 18 kwa ajili ya yatima na watoto wengine.
|