|
Mbunge aishukuru Serikali kwa kutajirisha wapiga kura wake
2006-12-28 16:21:42
Na Mwandishi wetu
Mbunge wa Ludewa , Profesa Raphael Mwalyosi, ameishukuru Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kupitia Hifadhi ya Taifa ya Chakula (SGR) Makambako wilayani Njombe kwa kufanikisha ununuzi wa kiasi kikubwa cha mahindi ya wananchi wilayani kwake.
Profesa Mwalyosi amesema hatua ya SGR Makambako kusogeza huduma za ununuzi wa mahindi kwa kufungua vituo vidogo vitatu katika vijiji vyya Mudindi-Liganga, Mlangali na Ludewa kumesaidia kupunguza malalamiko ya wakulima.
Profesa Mwalyosi amesema ana imani kwamba asilimia 70 ya Mahindi ambayo wakulima walihitaji kuyauza yamenunuliwa na SGR Makambako kwa bei nzuri.
Lakini pia Mbunge huyo amekishauri kituo hicho kuongeza uwezo wake kuhakikisha kiasi kikubwa cha mahindi ya wakulima hasa wale waishio vijijini yananunuliwa, badala ya kuwaachia walanguzi.
Mbunge huyo amesema hali hiyo kwa kiasi kikubwa imesaidia na kuchangia kuwakwamua wananchi hao na hali mbaya ya umasikini, na hivyo wengine kuhamasisha kuongeza jitihada katika shughuli za kuilimo.
Mbunge huyo amesema hayo alipozungumza na Alasiri hivi karibuni kueleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka mmoja, baada ya kumalizika kwa harakati za uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.
Mbunge huyo amesema hatua ya SGR Makambako kununua zaidi ya tani 3000 za mahindi kwa wakulima wenyewe badala ya kusubiri madalali kimeongeza imani ya wananchi hao kushiriki katika kilimo.
Kwa kweli wananchi wa Ludewa mwaka huu, walihamasika kwa kiasi kikubwa kushiriki shughuli za kilimo, na nina hakika wilaya yetu haiwezi kukumbwa na tatizo la chakula, wengi wameuza na kujiwekea akiba, amesema Mbunge huyo.
|