|
Dar watakiwa kukoromea uchafuzi wa mazingira
2007-01-04 17:46:34
Na Kiyao Hoza, Jijini
Wananchi Jijini Dar es Salaam wametakiwa kukemea tabia za uchafuzi wa mazingira zinazofanywa na baadhi ya watu na zinazoweza kuhatarisha afya zao.
Kukemea huko ni sambamba na kufuata sheria na kanuni za afya.
Hayo yamesema na Mganga Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Dk. Deo Mtasiwa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu vitendo vya uchafu vinavyochangia kasi ya ugonjwa wa kipindupindu.
Dk. Mtasiwa amezitaja tabia hizo kuwa ni kutapisha vyoo wakati wa mvua pamoja na kutiririsha maji machafu.
“Wananchi ndiyo wa kwanza kukemea tabia zozote za uchafu zinazoweza kuchangia kasi ya kuenea kwa magonjwa ya mlipuko, hususani kipindupindu,” amesema.
Akasema ili kuishinda vita hiyo ni lazima kila mwananchi awe mlinzi wa mwenzie kabla sheria haijashika mkondo wake.
Kadhalika amewataka viongozi na wataalamu walioko katika ngazi ya Kata kufanya kazi yao ili kuhakikisha kanuni na sheria hizo zinazingatiwa.
Wakati huo huo, Dk. Mtasiwa amesema jumla ya wagonjwa 11, wamelazwa katika kambi zote tatu za wilaya.
Kati yao wagonjwa waliolazwa, watano Ilala, Kinondoni ni wanne na Temeke wagonjwa wawili.
Ameyataja maeneo wanakotoka wagonjwa hao kuwa ni Buguruni, Vigunguti, Makurumla, Tandale, Mbagala Kiburugwa na Mkuranga.
|