|
Denti azolewa na daladala
2007-04-24 17:30:10
Na Moshi Lusonzo, Muhimbili
Mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari King`ongo, Mbaraka Ramadhani,15, amelazwa katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili, MOI baada ya kuzolewa na daladala.
Rama amepatwa na mkasa huo juzi, majira ya mchana katika eneo la Kimara Bucha, wakati akiendesha baiskeli ya miguu mitatu, maarufu kama guta, kufuata maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kwao.
Rama ameiambia Alasiri akiwa wodini pale katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili, MOI kuwa siku ya tukio, yeye alikuwa akiingia kwenye Barabara ya Morogoro na ndipo ghafla akastukia akigongwa na daladala aina ya kipanya.
Mwanzoni, anasema Rama kwamba alijaribu kuokoa maisha yake kwa kuruka toka kwenye guta, lakini kamwe hakuwahi. Badala yake akagongwa na kurushwa hadi mtaroni.
``Nilisukumwa kwa nguvu na lile daladala hadi nikaanguka mtaroni… baada ya hapo sielewi ni kitu gani kilichoendelea baada ya hapo kwani nilipoteza fahamu,`` akasema.
Katika tukio hilo, Rama ameumia vibaya kwa kuvunjika mguu na mkono wake wa kulia na pia amepatwa na majeraha tumboni.
Afisa Uhusiano wa MOI, Bw. Almas Jumaa, amesema mgonjwa huyo kwa sasa hali yake inaendelea vizuri na amelazwa wodi namba 17 jengo la Sewahaji.
|