|
Kinara wa unga adakwa Jijini
2007-04-27 17:49:16
Na Moshi Lusonzo, Polisi Kati
Wakati Serikali ikiwa kwenye vita kali dhidi ya madawa ya kulevya, mmoja wa wasambazaji wakubwa wa madawa hayo ametiwa mbaroni akiwa kwenye harakati za kuingia sokoni na kuanza kuisambaza bidhaa hiyo haramu iliyokuwa na thamani ya mamilioni ya pesa za Kibongo.
Taarifa za kipolisi zinasema jamaa huyo, ambaye inasemekana ni maarufu sana, alidakwa na mzigo wenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni 18.6.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, mzigo huo ulikuwa wa cocaine na tayari ulishapakiwa kwenye vifuko kabla ya kupelekwa sokoni kwa wasambazaji wadogo na baadaye wateja.
Mtu huyo ametajwa kwa jina la Mbarouk Ali Komesha almaarufu kama Muba, 32, ambaye ni mkazi wa Buguruni Malapa.
Imeelezwa kuwa mtuhumiwa alidakwa Jumanne wiki hii jioni katika maeneo ya Ilala Mchikichini.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, baada ya mtuhumiwa huyo kudakwa na kuhojiwa, alieleza kuwa madawa hayo alikuwa akijiandaa kuyapeleka sokoni. Hata hivyo hakutaja wateja wake ni akina nani na pia watu anaoshirikiana nao.
Imeelezwa kuwa tangu Aprili 24 alipotiwa mbaroni, mtuhumiwa huyo alikuwa akishikiliwa kwenye kituo cha polisi cha Kati wakati akiendelea kuhojiwa.
Hata hivyo, taarifa zaidi zinasema mtu huyo huenda akafikishwa katika mahakama ya Kisutu leo.
|