|
Mtoto afia kisimani
2007-04-30 15:52:36
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Watu wawili wamefariki dunia Jijini Dar es Salaam katika matukio mawili tofauti, akiwemo mtoto aliyetumbukia kisimani.
Kamanda wa mkoa wa kipolisi Ilala, Masindoki Masindoki, ameiambia Alasiri mapema leo kuwa mtoto huyo Mariam Shaban,4, alitumbukia kisimani saa 11.30 jioni jana huko Mongo la Ndege, Ukonga.
Akasema mtoto huyo alikuwa akicheza katika nyumba ya jirani na ndipo ghafla, akajikuta akitumbukia katika kisima na kufa.
Akasema mtoto huyo alifikwa na umauti baada ya kunywa maji mengi ndani ya kisima hicho.
Kamanda Masindoki akasema mwili wa mtoto huyo umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Amana Jijini.
Wakati huo huo, mwanamke mwenda kwa miguu anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 35 na 45 amefariki dunia baada ya kugongwa na gari.
Kamanda wa mkoa wa kipolisi Kinondoni, Jamal Rwambow, amesema mwanamke huyo alikumbwa na umauti jana, saa 2.00 usiku, wakati akivuka barabara ya Morogoro, eneo la Rombo.
Akasema dereva wa gari lilosababisha ajali hiyo aina ya Toyota Mark II, lenye namba za usajili T 544 ABC, alikimbia baada ya ajali hiyo.
Akasema polisi wanamsaka dereva huyo ambaye hakufahamika na mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya Mwananyama.
|