|
Benki yavunjwa, pesa kibao zakombwa
2007-06-11 18:40:34
Na Margareth Malisa, PST-Kibaha
Watu wasiofahamika wamevunja benki moja kule Kibaha usiku wa kuamkia leo na kukomba mapesa kibao, imeelezwa.
Taarifa ambazo mwandishi wa PST amezinasa toka kwenye vyanzo vya polisi zinasema watu hao, wakiwa na zana za kijambazi pamoja na silaha, waliweza kutinga kwenye eneo la benki inayodaiwa kuwa ni ya Posta na kukomba mapesa ambayo hadi tunakwenda mitamboni, haikuwa imefahamika rasmi ni kiasi gani.
``Bado tunaendelea kukusanya taarifa za tukio hili… baadaye tutawafahamisha kila kitu,`` amesema Afisa mmoja wa polisi kumueleza mwandishi wa PST leo asubuhi.
Kamanda wa Polisi mkoani Pwani hakuweza kupatikana ili kuzungumzia tukio hilo kutokana na maelezo kuwa yuko Chalinze kikazi.
Afisa mmoja wa juu katika Benki ya Posta alipoulizwa kuhusu tukio hilo, alijibu kwa kifupi kuwa bado hawana taarifa kamili za tukio. Hata hivyo aliahidi kufuatilia na kutoa taarifa kadri maelezo ya tukio hilo yatakavyopatikana.
|