|
`Pandeni miti kuzuia jangwa mkoani Pwani`
2007-06-12 16:26:10
Na Janneth Kiure, Kibaha
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Dk. Chiristine Ishengoma, amezitaka Taasisi na watu binafsi ambao wanatumia miti kwa wingi kujitahidi kupanda miti katika maeneo wanayoishi ili kuweza kupunguza uharibifu wa mazingira na hatimaye kupunguza hatari za kupoteza vyanzo vya maji na hatimaye kukaribisha jangwa.
Hayo yamesemwa wakati wa sherehe ya Siku ya Mazingira Duniani iliyofanyika katika Uwanja wa Shule ya Sekondari Bundikani mjini hapa.
Amesema kutokana na matumizi makubwa ya miti ikiwemo mbao, kuni na uchomaji wa mkaa wa zaidi ya magunia 40,000 kwa mwaka, Pwani iko katika hatari kubwa ya kugeuka jangwa.
Pia Dk. Ishengoma akawaagiza viongozi wa Halmashauri kuwahamasisha wananchi kupanda vitalu vingi vya miti ili kuhifadhi mazingira.
`Ni wajibu wao kuhakikisha kuwa wanatunza miti wanayopanda ili iweze kukua… wakizingatia hilo, mazingira yatakuwa bora siku zote na kuwa kivutio kikubwa kwa wakazi na hata kwa wageni watokao nje ya mkoa huu,` akasema Dk. Ishengoma.
Katika sherehe hizo, baadhi ya kata zilizawadiwa kwa kutunza vyema mazingira yao.
|