|
Bunge laanza, Spika achimbwa mkwara
2007-06-12 16:34:30
Na Kiyao Hoza, Dodoma
Kikao cha bunge la bajeti kimeanza leo mjini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine, Spika wa Bunge Mheshimiwa Samweli Sitta amewachimba mkwara waheshimiwa wasiozingatia kanuni.
Mkwara huo uliochimbwa na Spika, ni ule unaohusiana na kuzingatia kanuni za uendeshaji mambo ndani ya jengo hilo tukuka, hususan wakati wa kuendelea kwa shughuli mbalimbali za bunge.
Namna ilivyokuwa, ni kwamba Mheshimiwa Spika aliwaona wabunge kadhaa wakichezesha midomo yao kwa kutafuna pipi.
Hapo Mheshimiwa hakuwa na tatizo sana kuhusiana na hicho wanachokitafuna, akiwafagilia kwa kuwaeleza hao wanaotafuna kuwa kweli wanakwenda na wakati.
Mheshimiwa Spika hakuishia hapo. Baada ya kuwafagilia waliokuwa wakifaidi uhondo wa pipi, ndipo alipowakumbusha kanuni nyingine mojawapo kati ya zile zinazotoa miongozo mbalimbali bungeni.
Mheshimiwa Spika akasema kamwe, kanuni hazimpi ruhusa yeyote ndani ya kikao hicho kumung’unya pipi wakati akitoa hoja au kuuliza swali.
Baada ya kukumbushia jambo hilo, wabunge walitabasamu na wengine kuangua kicheko kabla ya kuendelea na kikao chao.
Awali, Spika Sitta aliwapa changamoto waheshimiwa wabunge kuwa waamke kwa kuuliza maswali ya nyongeza, kwani hadi lilipojibiwa swali la tatu na waheshimiwa mawaziri, hakukuwa na swali lolote la nyongeza.
`Inaonekana waheshimiwa bado mmelala… maana hakuna hata swali la nyongeza,` akasema Spika Sitta.
Mbunge mzoefu toka Jimbo la Kwela, Mheshimiwa Chrisant Mzindakaya, ndiye aliyejibu kivitendo changamoto hiyo ya Spika Sitta pale aliposimama na kuuliza swali la nyongeza, kwenda katika Wizara ya Utumishi wa Umma.
Wakati huohuo, joto la kutaka kusikia Serikali imejiandaa kuwafanyia nini wananchi wake katika mwaka wa fedha wa 2007 na 2008 limeanza kupanda baada ya kuanza kwa kikao hicho.
Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Zakia Meghji anatarajiwa kusoma bajeti ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha siku ya Alhamisi.
Shauku ya wengi waliozungumza na mwandishi wa habari hii ni kutaka kujua bajeti hiyo itawasaidiaje wananchi katika kuinua hali zao kiuchumi.
Kwa mujibu wa ratiba, Juni 14 mwaka huu baada ya kipindi cha maswali na majibu, Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Dk. Juma Ngasongwa atasoma taarifa yake kuhusu hali ya uchumi wa nchi kabla Waziri wa Fedha hajawasilisha bajeti ya nchi kwa mwaka ujao wa fedha .
Aidha, bajeti hiyo itawasilishwa kwa wakati mmoja na bajeti za mawaziri wa fedha wa nchi za Kenya na Uganda.
|