|
Mufti ataka Mama Kikwete aungwe mkono ujenzi wa Kituo cha Watoto Dar
2007-06-15 16:19:47
Na Mwandishi Wetu, Jijini
Mufti Mkuu wa Tanzania, Sheikh Issa Shaaban Simba, amewataka wananchi kujitokeza kumuunga mkono mke wa Rais, Mama Salma Kikwete,kwenye kuchangia ujenzi wa shule maalum ya michezo kwa yatima na watoto wanaoishi katika mazingira magumu.
Sheikh Simba ambaye ni mlezi wa kamati ya ujenzi, aliwahimiza wananchi kujitokeza kuchangia kwenye hafla ya chakula cha hisani itakayofanyika leo katika viwanja vya Karimjee Hall jijini Dar es Salaam.
Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari, Mufti aliwataka Watanzania wote kumuunga mkono Mama Kikwete ambaye anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Alisema shule hiyo ni ya kwanza ya aina yake itakayoshughulikia mchakato wa michezo mashuleni kwa kuwatayarisha vijana kimichezo kitaifa na kimataifa , inajengwa kwa gharama ya Sh. milioni 80.
` Mama Kikwete kuwa mgeni rasmi katika hafla hii ni jambo la faraja kubwa katika harakati za kuinua michezo Tanzania na hasa ikizingatiwa ni Mama wa familia na ni mwanamichezo pia.Hivyo nawaomba Watanzania wote wenye mapenzi mema kimichezo na kijamii tujitokeze siku hiyo ili tuchangie na kumuunga mkono`
Alikumbusha kuwa hafla hiyo hufanyika sambamba na siku maalum ya Mtoto wa Afrika inayoazimishwa barani kote Juni 16 kila mwaka.
`Juni 16 ni siku ya Mtoto wa Afrika, hivyo tuwajali watoto wetu kwa kuwatayarishia urithi wa elimu kimichezo ili michezo ije iwape ajira hapo baadaye,` ilisema taarifa ya Mufti.
|