|
Lori lafumua daladala Dar…watano hoi Mlinzi agongwa na kufa akifungua geti
2007-08-25 19:16:04
Na Kiyao Hoza, Jijini
Watu sita wamejeruhiwa vibaya baada ya gari aina ya daladala waliyokuwa wakisafiria kugongwa na lori Jijini Dar es Slaam.
Kamanda wa mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Jamal Rwambow amesema ajali hiyo imetokea mishale ya saa 4:00 usiku wa kuamkia leo katika barabara ya Morogoro eneo la Kimara.
Amesema magari yaliyohusika katika ajali hiyo yote yalikuwa yakitokea Kimara kuelekea Ubungo.
Akisimulia tukio hilo, Kamanda Rwambow amesema ajali hiyo imetokea baada ya lori lililokuwa liko kwenye mwendo kuigonga daladala hiyo kwa nyuma.
Amesema daladala hiyo iliyohusika katika ajali ina namba T733 AFN Toyota Hiace iliyokuwa ikiendeshwa na derea Abdul Kweka, 30 wakati lori hilo lina namba T130 AGM ambalo dereva wake aliingia mitini baada ya ajali.
Kamanda amewataja majeruhi kuwa ni Elly Shuma, 40, Jenny Augustino, 18, Nurdin Katala, 29, Salehe Kala, 42 na Arenes Mgogo, 38 ambao wote wamelazwa katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Wakati huohuo mtu mmoja ambaye ametajwa kuwa ni mlinzi, amefariki dunia baada ya kugongwa na gari wakati akilifungulia geti.
Kamanda Rwambow amemtaja marehemu kuwa ni Mohamed Abdul, 23 mkazi wa Kinondoni Moscow.
Amesema tukio hilo limetokea Kinondoni Studio usiku wa kuamkia leo kwenye majira ya saa 2:45.
Amesema dereva wa gari hilo alikimbia baada ya ajali na mwili wa marehemu umehifadhiwa katika chumba cha maiti cha hospitali ya Mwananyamala.
|