|
Hali ya afya ya Mpakanjia si shwari
2007-08-25 19:21:22
Na Mwandishi wetu, Jijini
Kuna taarifa kuwa mfanyabiashara maarufu wa Jijini Dar es Salaam, Mohamed Mpakanjia amekumbwa na kile kile kilichomuua mkewe, marehemu Amina Chifupa.
Baadhi ya watu walio karibu na familia hiyo wamelidokeza gazeti hili kwamba dalili alizokuwa nazo marehemu Amina siku za mwanzo za ugonjwa wake, tayari zimeanza kuonekana kwa mumewe.
Baadhi ya watu wamedai kuwa kutokana na hali yake kutoridhisha, sasa Mpakanjia kalazwa katika Hospitali Kuu ya Jeshi iliyopo Lugalo Jijini.
Amesema namna ya ugonjwa unaomsumbua Mpakanjia ulivyo ni fumbo linalowashangaza hata wao, hasa kutokana na ukweli kuwa dalili za ugonjwa wenyewe ni kama zile alizowahi kuwa nazo mkewe, marehemu Amina Chifupa.
``Hali yake si nzuri. Hivi sasa, hata anachokizungumza hakieleweki… amedhoofu mno na hata kusimama mwenyewe hawezi. Kwakweli anasikitisha sana,`` akasema ndugu huyo.
Dalili kama hizo pia zililipotiwa kujitokeza kwa aliyekuwa mkewe, marehemu Amina Chifupa, ambaye alifariki dunia Juni 26 mwaka huu katika hospitali hiyo hiyo ya Lugalo.
Kabla ya kifo chake, marehemu Amina aliripotiwa kuzungumza mambo yasiyoeleweka na mwili wake kudhoofu kiasi cha kushindwa kuinuka.
Baadhi ya ndugu wa mfanyabiashara huyo wamedai Bw. Mpakanjia alilazwa hospitalini hapo mwanzoni mwa wiki hii.
Akizungumzia kile kinachomsibu Mpakanjia, ndugu mmoja wa mfanyabiashara huyo amesema mgonjwa wao hivi sasa ana hali mbaya na kwamba hata kula kwa mikono yake hawezi.
Amesema amewekewa mirija kwa ajili ya kumsaidia huku madakitari wakijitahidi kumhudumia.
|