|
Gari Dar lateketea kwa moto, dereva atimka
2008-02-26 15:50:01
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Gari dogo aina ya Hyundai lenye namba za usajili T 624 AJE limeteketea kwa moto katika barabara ya Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, Masindoki Masindoki amesema gari hilo limeshika moto mishale ya saa 4:00 usiku wa kuamkia leo.
Amesema lilikuwa linaendeshwa na Bw. Msemwa Mohamed ambaye ni fundi aliyepewa kulitengeneza.
Kamanda Masindoki amesema Bw. Mohamed alikuwa akiendesha gari hilo kuelekea nyumbani kwake, lakini baada ya gari kushika moto alikimbia na kuliacha.
Akasema gari hilo ni mali ya George Mpondela ambaye wakati gari lake likitetea alikuwa safarini.
Kamanda Masindoki amesema chanzo cha moto huo hakijafahamika na kuwa mabaki yake yamehifadhiwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Wakati huo huo Jeshi la Polisi linawashikilia watu 11 waliokamatwa wakiwa na kete 88 za bangi.
Kaimu Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Pius Sheka amesema watu walikamatwa jana kuanzia mishale ya 4:00 asubuhi hadi saa 8:00 mchana wakati Polisi wakifanya msako.
Amesema msako huo ulifanywa katika maeneo ya Kigogo, Sinza na Mburahati.
Amewataja baadhi ya watuhumiwa hao kuwa ni Idda Mbwana, 28, Geofrey Kiwane, 32, Stiphen Mwita, 22, Antony Joseph, 29 na Seuli Lesiaga, 25.
|