|
Manispaa ya Ilala kujifunza mbinu za kuinua mapato
2008-05-09 19:19:36
Na Grace Chilongola, PST - Jijini
Manispaa ya Ilala imekuwa miongoni mwa halmashauri zinazoshirikiana na Taasisi ya Ushirikiano wa Maendeleo katika Serikali za Mitaa Kusini mwa Jangwa la Sahara, Municipal Development Partnership na hivyo kujipa uwezekano wa kujifunza mbinu shirikishi za kuinua mapato ya halmashauri yake.
Hayo yamesemwa na Mratibu wa TASAF katika manispaa ya Ilala, Bw. Renatus Kihongo, wakati alipokuwa akizungumza na PST kuhusu mradi wa mafunzo ya mbinu shirikishi kutoka Latin Amerika, ambazo zinawezesha kuinua mapato na hatimaye kutoa huduma bora kwa wananchi.
Amesema mradi huo unafadhiliwa na Benki ya dunia , Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi (UN Habitat) na Serikali ya Uholanzi ambapo nchini Tanzania manispaa ya Ilala pamoja na Jiji la Mbeya linashiriki.
Bw. Kihongo amesema mfano wa mbinu shiriki zinazotumiwa katika ushirikiano huo ni pamoja na kuwashirikisha ama kukutana na wafanyabiashara kuzungumzia jinsi kodi zao zinavyotumika na kisha kupata maoni yao.
Amesema kabla ya mwisho wa mwezi huu, utafanyika mkutano wa kuandaa Mpango kazi wa Mradi wa mafunzo ya mbinu shirikishi nchini Ethiopia ambapo manispaa ya Ilala itatuma mwakilishi wake.
Manispaa ya Ilala iliingia kwenye ushirikiano huo mwaka 2006 wakati mpango huo ulianza tangu mwaka 1998 na kwamba makao makuu ya ushirikiano huo yapo katika Jiji la Harare nchi Zimbabwe.
|