|
Simba SC kwawaka
2008-05-15 19:49:51
By Mwandishi wetu, Msimbazi
Baadhi ya wanachama wa klabu ya Simba, wanaotaka mkutano mkuu, wameunga mkono hatua ya Msajili wa Vyama vya Michezo Manispaa ya Ilala, kuubana uongozi kwa lengo la kuushinikiza kufanyika kwa mkutano huo.
Wanachama wa Simba wanadai kuitishwa kwa mkutano mkuu mwezi huu, lakini uongozi umesema wazi kuwa uwezekano wa mkutano huo kufanyika mwezi huu haupo, na badala yake wamependekeza ufanyike Juni mwaka huu.
Kwa kipindi kirefu wanachama wa Simba wamekua wakiushinikiza uongozi wao kuitisha mkutano bila mfanikio, lakini jana bosi wa michezo wa Manispaa ya Ilala Penina Maduhu, amesema atauweka kitimoto uongozi kujua sababu za kuwanyima haki ya mkutano wanachama wenye dhamana ya maamuzi na klabu hiyo.
Wakiongea na Alasiri makao makuu ya klabu hiyo Msimbazi, jijini Dar es Salaam, wanachama wamesema suala la mkutano ni haki ya wanachama na wanashangazwa uongozi wao kulifumbia macho suala hilo.
Juma Abdallah akiongea kwa niaba ya wanachama wenzake, alisema kuwa hatua ya serikali ya kuhoji kuchelewa kwa mkutano huo ni hatua nzuri na inayolenga kujali haki ya wanachama.
``Kipindi kirefu kimepita bila kufanyika mkutano, nadhani hakuna sababu ya kuchelewa, tunamwomba msajili auambia uongozi kuitisha uchaguzi mapema,`` alisema.
Abdallah amesema kuwa, kuna mambo mengi yamepita hivyo muda umefika ili kuelezana yaliyotokea.
Mwanachama mwingine Kassim Juma, amemuomba msajili kutokubali utetezi wa uongozi wao katika kuitisha mkutano, kwa vile tabia ya kupiga danadana kufanyika kwa mkutano umekuwa ni utamaduni wao.
``Tumedai sana kufanyika kwa uchaguzi, sasa wanasema mwezi huu hautafanyika mpaka Juni, na pengine inaweza kufika na ikapita bila mkutano kufanyika,`` alisema mwanachama huyo.
|