|
Serikali, Lions Club kushirikiana
2006-10-28 08:07:43
Na Mwandishi wetu
Serikali imeahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Lions Club ili taasisi hiyo iendelee kutoa na kusambaza huduma za kijamii kwa wananchi wengi zaidi.
Ahadi hiyo ilitolewa juzi na Rais Jakaya Kikwete wakati wa mazungumzo yake na Rais wa Lions Club, Bw. Jimmy Ross, Ikulu jijini Dar es Salaam ambapo Rais alipewa medani ya Lions Club.
Alisema kuwa serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na Lions Club kwa wananchi nchini, hususani wale wanaokabiliwa na matatizo mbalimbali ya kiafya wakiwemo watu wenye matatizo ya macho.
Rais Kikwete alisema serikali inakaribisha michango mbalimbali inayolenga katika kusaidia juhudi za serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi.
Mazungumzo hayo pia yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa ngazi ya juu wa Lions Club wakiwemo Manoja Shah, Hashim Nkya, Safder Jaffer na Yusuf Mushi.
Ross alisema taasisi yake imedhamiria kupanua wigo wa utoaji wa huduma zake, ikiwa ni pamoja na kuanzisha hospitali kubwa itakayotoa huduma ya macho hususani kwa wananchi wa vijijini.
Alimweleza Rais kwamba, Lions Club hivi sasa inaandaa mpango utakaoiwezesha asasi hiyo kusaidia juhudi za serikali katika kuwapatia wananchi wake huduma bora za afya.
Aliitaja mipango hiyo kuwa ni pamoja na kuleta nchini vifaa vya matibabu, ambapo pia mafunzo ya matumizi ya vifaa hivyo, ukarabati wake yatatolewa pamoja na vipuri vyake.
Bw. Ross alisema kwamba taasisi yake inaandaa pia taratibu zitakazoziwezesha hospitali za hapa nchini kuwa na uhusiano na hospitali za nchi mbalimbali lengo likiwa kubadilishana uzoefu wa utoaji wa huduma za kiafya.
Akiwa nchini, Rais huyo wa Lions Club alipata nafasi ya kutembelea miradi mbalimbali inayoendeshwa na asasi hiyo.
Alikutana pia na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Profesa David Mwakyusa.
|