|
Wastaafu EAC walumbana
2008-05-16 10:06:05
Na Lucy Lyatuu na Ellen Manyangu
Wastaafu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamelalamikia kitendo cha kuchangishwa fedha Sh. milioni 120 kwa wastaafu hao kwa madai ya kufungua kesi katika mahakama ya nje ya nchi.
Uchangishwaji huo unadaiwa kufanywa na aliyekuwa Mwenyekiti wao, Bw. Alfred Kinyondo, ambaye naye alisema alizitumia fedha hizo kwa kufungua ofisi.
Malalamiko dhidi ya Bw. Kinyondo yalitolewa na mmoja wa wawakilishi wao, Bw. Ahmed Kabunga, wakati akizungumza katika viwanja vya Mnazi Mmoja jana jijini Dar es Salaam.
Alisema Bw. Kinyondo aliwachangisha fedha wastaafu hao kwa nia ya kufungua kesi nje ya nchi akiwa na imani kwamba huko ataweza kupata ufumbuzi wa madai yao.
``Hivi ana kigugumizi gani, mbona haongelei juu ya kesi hiyo, wastaafu hamlioni hilo?`` Alihoji Bw. Kabunga.
Aliongeza kuwa Bw. Kinyondo aliwachangisha wafanyakazi hao kiasi cha Sh. milioni 120 kwa madai kuwa atafungua kesi nje ya nchi kwa kuwa ndiko haki ya wastaafu hao inakoweza kupatikana.
Hata hivyo, alisema Bw. Kinyondo amekuwa akifanya mambo mengi ya kuwachanganya wastaafu hao ikiwa ni pamoja na kuandika barua kwa Rais Jakaya Kikwete akiomba kupatiwa Sh. milioni 20 ili kila mstaafu aweze kujikimu na maisha, jambo ambalo hawajui mwisho wake.
Aidha alisema barua hiyo na nyingine hazikuwa na ujumbe wa maana bali zilianika udhaifu wake na tofauti za wastaafu mbele ya wale wanaopingana nao.
Aliwataka wastaafu hao kufahamu kuwa madhumuni ya umoja wao ni kuweka nguvu pamoja ili kudai haki zao dhidi ya serikali.
``Inasikitisha na inafedhehesha kuwa mvutano na uhasama kati ya wastaafu bado umezidi kukua na kupunguza nguvu za umoja dhidi ya mdaiwa ambae ni serikali,`` alisema Bw. Kabunga.
Alisema ni vema ikazingatiwa kuwa kesi ya madai iko mikononi mwao na kwamba wanawawakilisha wastaafu wote bila kujali itikadi au kikundi fulani, haki zao zitalipwa kwa nguvu za sheria na si vinginevyo.
Akizungumzia madai hayo, Bw. Kinyondo alisema fedha zilizochangishwa ni Sh. milioni 15 na sio milioni 120 kama ambavyo inadaiwa na wastaafu.
Alisema fedha hizo alizochangisha alizitumia kwa kufungua ofisi kwa kuwa wastaafu hao walikuwa hawana sehemu ambayo wangeweza kuitumia kufikisha ujumbe wao.
Kuhusu kufungua kesi nje ya nchi alisema tayari wameshapata mtu anayeratibu shughuli hizo huko nchini Ujerumani na kwamba pindi akikamilisha atatoa ufafanuzi kwa wastaafu wenzake.
|