|
DRC imetakiwa kuimarisha ulinzi mpakani
2006-10-24 14:10:09
Na Radio One Habari
Jeshi la polisi mkoani Rukwa limeitaka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo kuthibiti na kuimarisha ulinzi mpakani ili kudhibiti uvukaji holela wa mara kwa mara wa wananchi wake kupitia mwambao wa Ziwa Tanganyika upande wa Tanzania na kufanya uporaji.
Kaimu wa kamanda wa polisi mkoa wa Rukwa Bw. Germanus Mponguliana ametoa kauli hiyo baada ya mali za wananchi wa wilaya ya Nkasi zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 42 kuporwa na majambazi mwezi uliopita na kupatikana zikiwa zimetelekezwa katika Jamhuri hiyo.
Ametaja mali zilizoporwa kuwa ni pamoja na radio, seti za televisheni, viti, galoni za mafuta, injini za boti, betri za magari na magodoro.
Bw. Mponguliana amesema wengi wa majambazi wana wanasadikiwa kuwa ni askari wa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo ambao huingia nchini kupitia mwambao wa ziwa Tanganyika na kufanya uporaji wa mali na bidhaa mbalimbali za wakazi wa mwambao wa ziwa hilo upande wa Tanzania.
|