|
Tatizo la msongamano wa wafungwa na mahabusu linaweza kupungua-Mungai
2006-10-24 14:11:04
Na Radio One Habari
Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Joseph Mungai ameshauri vyombo vya dola, hasa vya Polisi, Magereza na Mahakama kufanya kazi kwa ushirikiano ili kusaidia kupunguza msongamano wa mahabusu na wafungwa magerezani.
Mhe. Mungai ametoa ushauri huo wakati akizungumza mjini Iringa na viongozi na watumishi wa Idara za uhamiaji, Magereza na Jeshi la zimamoto zilizo chini ya wizara yake.
Amesema tatizo la msongamano wa wafungwa na mahabusu linaweza kupungua iwapo kamati za kufuatilia mashauri zitafanya kazi ipasavyo na kwa haraka zaidi.
Mhe. Mungai amesema makosa ya baadhi ya mahabusu yangeweza kushughulikiwa wakiwa nje ya magereza kama vyombo vya dola vitaimarisha ushirikiano katika kazi zao.
Waziri Mungai ameahidi kuwasilisha mapendekezo serikalini ili iongeze mgao wa fedha kwa ajili ya kuboresha huduma za wizara yake kadri mapato ya serikali yanavyoongezeka.
|