|
Rais kuwa mgeni rasmi katika Baraza la Eid
2006-10-24 14:14:40
Na Radio One Habari
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amewataka Waislam nchini kuendeleza na kudumisha mema yote waliyoyafanya wakati wa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Rais Kikwete amesema kumalizika kwa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kusiwe mwanzo wa kurejea katika maovu na kuhatarisha amani.
Alikuwa akizungumza baada ya swala ya Eid-el-Fitr iliyoswaliwa katika msikiti wa Kwa-Mtoro jijini Dar es Salaam leo. Rais Kikwete anakwenda Arusha ambako atakuwa mgeni rasmi katika Baraza la Eid leo jioni.
Awali Sheikh Abdallah Mohamed Juma wa msikiti wa Kwa-Mtoro aliwaasa Waislam kutumia siku hii ya iddi kusaidiana na kuhurumiana.
Naye Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein ameungana na Waislam wa msikiti wa Tambaza-Upanga jijini Dar es Salaam kusali swala ya Iddi.
Akizungumza katika swala hiyo Sheikh Ahmed Saidi Khalili wa msikiti wa Tambaza alitoa wito kwa Waislam kutotumia siku ya leo kutenda maovu na kuwasaidia wasio na uwezo.
|