|
Wauguzi Bugando wameilalamikia serikali
2006-10-25 14:53:21
Na Radio One Habari
Uongozi na wafanyakazi wa hospitali ya rufaa ya Bugando Mkoani Mwanza wameilalamikia Serikali Kuu kwa kukiuka baadhi ya vipengele vilivyoko katika sheria na mkataba wa ajira.
Wafanyakazi hao wakiwemo Madaktari, Wauguzi na Wakunga wametoa malalamiko yao walipozungumza na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Prof. David Mwakyusa juu ya matatizo yanayowakabili hospitalini hapo.
Kupitia risala yao na hotuba ya Mkurugenzi wa hospitali hiyo Dk. Charles Majinge, wafanyakazi hao walivitaja baadhi ya vipengele vinayoendelea kukiukwa na serikali kuwa ni pamoja na kile kinachotaja muda wa mfanyakazi kuthibitishwa kazini na kupandishwa daraja.
Katika risala yao wamedai kuwa baadhi ya wafanyakazi, karibu mia moja wanakaribia muda wa kustaafu kazi kabla ya kupandishwa madaraja na wengi hawajathibitishwa kazini.
Kwa upande wake Prof. Mwakyusa ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za kuadhimisha miaka 35 tangu kuanzishwa kwa huduma za matibabu katika hospitali hiyo, aliahidi kulifanyia kazi mapema suala hilo.
|