|
Kina cha maji katika Ziwa Victoria chapungua
2006-11-01 16:25:54
Na Radio One Habari
Kina cha maji katika Ziwa Victoria kimefikia mita 1131.7 juu ya usawa wa bahari hadi kufikia tarehe 21 mwezi uliopita ikilinganishwa na kina cha wastani cha muda mrefu ambacho ni mita 1132.2
Naibu Waziri wa Maji Mheshimiwa Shamsa Mwangunga ameliambia bunge kuwa hali hiyo imesababisha athari mbalimbali zikiwemo meli kushindwa kutia nanga na baadhi ya vituo vya maji kufungwa au kuhamishwa katika miji ya Mwanza, Bukoba na Musoma.
Akijibu swali la mbunge wa viti maalum Mheshimiwa Kidawa Salehe, Naibu Waziri ametaja sababu za kupungua kwa kina cha maji katika ziwa Victoria kuwa ni pamoja na ukame wa miaka mitatu mfululizo, kupungua kwa maji ya mvua katika maeneo yanayozunguka ziwa na matumizi makubwa ya maji ya ziwa hilo.
Mheshimiwa Mwangunga amesema ili kutafuta ufumbuzi wa tatizo la kupungua kwa kina cha maji katika ziwa Victoria nchi zote za Jumuia ya Afrika Mashariki, Tanzania, Kenya na Uganda pamoja na Rwanda zinaandaa mpango wa pamoja wa utekelezaji wa mradi wa hifadhi ya mazingira ya ziwa hilo awamu ya pili kuanzia mwishoni mwa mwaka ujao.
|