|
Madiwani wapewa elimu ya uendeshaji na utunzaji wa masoko
2007-04-23 18:52:48
Na Radio One Habari
Mpango wa Uboreshaji wa Mifumo ya Masoko ya Mazao ya Kilimo Vijijini umeanza kutoa elimu kwa madiwani juu ya uendeshaji na utunzaji wa masoko, barabara na maghala ili miundombinu hiyo iweze kuwa endelevu baada ya wafadhili kujitoa.
Mpango huo ambao unatekelezwa katika kanda mbili hapa nchini zenye mikoa minane unahusisha maeneo makuu manne ambayo ni pamoja na kukuza sera nzuri za soko la mazao ya kilimo na kuwawezesha wazalishaji wadogo na wa kati kwa kuwahakikishia mifumo mizuri ya masoko.
Mhandisi wa mpango huo Kanda ya Kusini Bwana Jacob Mwambene amezungumza hayo wakati wa mafunzo ya madiwani yaliyofanyika jijini Mbeya.
Bwana Mwambene ametaja maeneo mengine yaliyolengwa na mpango huo kuwa ni kuwajengea uwezo wa kifedha wazalishaji wadogo kwa kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo yao na kuimarisha miundombinu mbalimbali inayohusiana na masoko ya mazao ya kilimo.
|