|
Serikali inafanya juhudi kila upande unafaidika na muungano
2007-04-23 18:56:22
Na Radio One Habari
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia masuala ya muungano Dk. Hussein Mwinyi amesema serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inafanya jitihada kuona kila upande wa muungano unafaidika na matunda ya muungano huo.
Dk. Mwinyi amesema hayo mjini Zanzabar alipozungumza na waandishi wa habari juu ya masuala mbalimbali wakati Tanzania ikiadhimisha miaka 43 ya muungano.
Amesema hatua za makusudi zimechukuliwa kuhakikisha miradi ya pamoja inaandaliwa na kutekelezwa pande zote za muungano kama mfuko wa maendeleo ya jamii-TASAF na hivyo kwa kiasi kikubwa kuleta mafanikio na kuonesha mwelekeo wa kugawana matunda kwa pande zote mbili.
Aidha kuhusu dhana ya baadhi ya wananchi kuwa matunda ya muungano yanapendelea zaidi upande mmoja Dk. Mwinyi amesema madai hayo sio kweli na kamwe hayana msingi wowote.
|