|
Mpango wa kukabiliana na ugonjwa wa macho umeandaliwa
2007-08-25 19:13:04
Na Radio One Habari
Serikali kwa kushirikiana na wahisani wa nje katika sekta ya afya wameandaa mpango maalum wa kukabiliana na tatizo la ugonjwa wa macho na magonjwa mengine yanayoathiri macho.
Mratibu wa huduma ya macho kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Dakta Grace Saguti amesema hayo mjini Moshi mkoani Kilimanjaro wakati akifungua mkutano wa wataalam wa macho kwa niaba ya Naibu Waziri wa wizara hiyo Dakta Aisha Kigoda.
Amesema tatizo la magonjwa ya macho limekuwa likiwakumba watu wengi na kwamba mkutano huo unaoshirikisha wataalam wa macho kutoka nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika- OSEA, utajadili mpango wa kutokomeza magonjwa ya macho ifikapo mwaka 2020.
Naye daktari bingwa wa magonjwa wa macho katika kitengo cha watoto kutoka hospitali ya rufaa ya KCMC Moshi Dakta Bernadetta Robert amesema mbali na kuwekeana mipango hiyo mkutano huo umelenga kujadili namna ya kutokomeza kabisa magonjwa ya Trakoma, mtoto wa jicho, upofu kwa watoto na yale yanayotibiwa kwa miwani.
Mkutano huo wa siku mbili unahudhuriwa na madaktari bingwa kutoka Tanzania, Malawi, Ethiopia, Rwanda, Kenya, Uganda, Afrika Kusini , Zambia, Kongo, Uingereza na Marekani.
|