|
Serikali kuanzisha maghala ya kuhifadhia mazao nchini kote
2008-03-17 17:52:03
Na Radio One Habari
Serikali imepanga kuanzisha maghala ya kuhifadhi mazao kote nchini ili yasaidie kuongeza bei ya mazao na kuharakisha maendeleo ya wakulima na ukuaji uchumi kwa jumla.
Aidha katika kuimarisha sekta ya kilimo serikali imeanza kuzungumza na makampuni ya nje yatakayoweza kujenga viwanda vya kutengeneza zana za kilimo yakiwemo matrekta madogo na makubwa na pembejeo.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Profesa Peter Msolla wakati akizungumza na wakulima wa kijiji cha Ruaha Mbuyuni katika wilaya ya Kilolo mkoani Iringa.
Amesema chini ya mkakati huo serikali itapenda kuona wakulima wengi wanatumia zana za kisasa ili kuacha jembe la mkono na kuzalisha chakula cha kutosha kwa matumizi ya ndani na kupata ziada ya kuuza nje ya nchi.
Mkoa wa Iringa ni miongoni mwa mikoa minne pamoja na Mbeya, Rukwa na Ruvuma ambayo miaka ya nyuma ilikuwa maarufu kwa uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula na hasa mahindi.
|