|
Chuo kikuu Mkwawa wasomea kwenye bwalo
2008-03-23 15:20:30
Na Radio One Habari
Chuo kikuu kishiriki cha Mkwawa mkoani Iringa kinakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa hali ambayo imekifanya kutumia bwalo la chakula kwa shughuli za masomo.
Mkuu wa chuo hicho Profesa Philemon Mushi amesema matumizi ya bwalo la chakula kwa masomo kwa wanafunzi 350 yanaleta usumbufu kwani wakati wa kula wanachuo wengine wanahitaji kulitumia bwalo hilo kwa masomo.
Profesa Mushi amemwambia Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Jumanne Maghembe kuwa ili kukabiliana na matatizo yanayokikabili, chuo kimeomba zaidi ya shilingi bilioni 15.1 kwa ajili ya shughuli za maendeleo, mishahara na matumizi ya kawaida.
Ameyataja matatizo mengine yanayohitaji kushughulikwa kuwa ni pamoja uhaba wa walimu, upungufu wa vifaa vya teknolojia ya habari na mawasiliano na ukarabati wa barabara kuingia chuoni unaohitaji zaidi ya shilingi milioni-560.
|